WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa mkutano wa wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kujadili mapitio ya sera na mafunzo ya mwaka 2014 na mabadiliko ya mitaala ya elimu nchini.
Hayo yamesemwa leo Septemba
25,2022 na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Prof Adolf Mkenda
wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema kuwa mkutano huo
unatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 26 hadi 28 Septemba 2022 Jijini Dodoma.
Waziri Mkenda amesema kuwa
Mkutano huo unajumuisha, Wahadhiri, Waajiri, Wadau wa Maendeleo, Taasisi za
umma na Binafsi, Taasisi za Dini, Taasisi zinahusika na uendelezaji wa lugha,
Wabunge, Wajumbe toka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Taasisi zisizo za Kiserikali,
Jumuiya za kitaaluma, na Taasisi za Sayansi na Utafiti.
”Lengo la Mkutano huo ni kujadili
Mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 na Mabadiliko ya Mitaa ya
Elimu msingi ambapo timu ya Zanzibar inayopitia Sera na mitaala itaongozwa na
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na wajumbe wengine kutoka
Zanzibar”amesema Waziri Mkenda
Amesema kuwa majadiliano hayo
yatatokana na hatua iliyofikiwa na mapitio hayo kupitia kamati maalumu
zilizopewa majukumu hayo.
Aidha Waziri Mkenda amesema kuwa
Serikali imezindua tuzo za waandishi bunifu zijulikanazo kama Tuzo za Mwalimu
Nyerere, hivyo awakumbusha Waandishi Bunifu wa Riwaya na Mashairi kuwasilisha
maandiko yao ili kuwania tuzo hizo.
”Mwisho wa kupokea Mawasilisho
hayo ni Novemba 30, 2022 ambapo kwa taarifa zaidi kuhusu tuzo hizo na maulizo
wanaweza kufuatilia katika akaunti maalumu za mitandao ya kijamii za tuzo
Nyerere au mitandao na tovuti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na
Taasisi ya Elimu Tanzania-TET kwa anuani ya tuzonyerere@tie.go.tz”amesisitiza
Prof.Mkenda
0 Comments