https://monetag.com/?ref_id=TTIb Breaking News: Watu watano wapoteza maisha kwa ajali Kibaigwa Dodoma. | Muungwana BLOG

Breaking News: Watu watano wapoteza maisha kwa ajali Kibaigwa Dodoma.


Na Ezekiel Mtonyole, Dodoma.




Watu watano (5)wamepoteza maisha na wengine wawili kujeruhiwa katika ajali ya barabarani iliyotokea alfajili ya Leo katika eneo la Kibaigwa Mkoani Dodoma iliyohusisha magari mawili Toyota Noah na Lori la mizigo.

Akizungumza akiwa katika eneo la ajali Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, SACP Gilles Muroto amesema ajali hiyo imehusisha gari aina ya Noah T. 897 DCC toka Morogoro kwenda Dodoma na Lori la mizigo lenye namba T. 183 AXC lililokuwa likitoka Dodoma kuelekea Dar es saalam.

Kamanda Muroto akitoa taarifa za awali amesema ajali hiyo imesababishwa na uzembe wa dereva wa Lori ambaye alikimbia baada ya ajali hiyo aliyeingia barabarani toka upande wapili bila kuchukua tahadhari na kusababisha ajali hiyo.

" Ni kwamba huyu mwenye lori ambaye baada ya kusababisha ajali hiyo amekimbia na tunaendelea kumtafuta alitoka upande wa pili wa barabara na kuingia barabarani bila tahadhari na kusababisha ajali hii" amesema Kamanda Muroto.

Kamanda Muroto amesema majeruhi wawili wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Wilaya ya Kongwa na miili hiyo imehifadhiwa katika hospitali hiyo kwa ajili ya utambuzi.

Ametoa tahadhari kwa madereva wote kuwa makini wawapo barabarani ili kuepusha ajali Kama hizo ambazo zimekuwa zikigharimu maisha ya watanzania wasiona hatia.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Binilith Mahenge amefika katika eneo la ajali na kuzungumza na wananchi katika eneo hilo sambamba na kuwapa pole ndugu na jamaa kwa ajali hiyo.

Ambapo amesisitiza kila mmoja katika eneo lake kuchukua tahadhari juu ya kutokea kwa ajali baya kama hizo na kuwataka Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma na Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Deo Ndejembi kutekeleza maagizo ya kuondoa pakingi za magari makubwa katika sehemu zenye misongamano ya watu Kama Kibaigwa na Chalinze nyama ili kuepusha ajali Kama hizo.