Marekani yaathirika zaidi na virusi vya corona


Marekani imerekodi maambukizi mapya 53,000 ya virusi vya corona wakati janga hilo likiongezeka nchini humo, lakini upunguaji   barani Ulaya umesababisha Uingereza kutangaza kuondolewa kwa sheria yake ya karantini.

Wakati Ulaya  inaonekana  kusogea  katika  ukurasa mpya  katika mzozo  huu  mkubwa  wa  kiafya  katika  historia ya  dunia, wasafiri wanaowasili  nchini  Uingereza  kutoka  Ujerumani, Ufaransa, Uhispania  na  Italia  hawatalazimika  kujitengwa kuanzia  Julai 10.

Ugonjwa  wa  COVID-19  ukigusa  karibu  kila  nchi  hapa  duniani, ugonjwa  huo unaosababishwa  na  virusi , umefikia watu karibu milioni 10.7 na  kusababisha  vifo  vya  watu 516,000 duniani  kote, na  kuathirika  uchumi  ambao  ulikuwa  ukikua  kwa  kiasi  kikubwa na  kusababisha  maisha  ya  jamii  kusimama  kabisa.

Mkurugenzi wa taasisi ya taifa ya magonjwa ya kuambukiza nchini Marekani Anthony Fauci akijitayarisha kutoa maelezo katika kamati ya afya ya seneti.

Wakati  eneo  kubwa  la  dunia  likirejea  katika  hali  ya  kawaida , Marekani  imefikia kesi  zaidi  ya  50,000  za  maambukizi  mapya jana kwa  mara  ya  pili  katika  siku  mbili, ikionesha  hali  mbaya katika  sherehe  zijazo  za  uhuru  wa  nchi  hiyo.

Kwa  hivi  sasa  ikiwa  ndio  kitovu  cha  janga  hili, nchi  hiyo imerekodi  karibu vifo 129,000 kutoka  zaidi  ya  kesi milioni  2.7 za maambukizi. Inatarajiwa  kufikia  idadi  ya  kesi milioni 3  za maambukizi  wiki  ijayo.

Ulaya yaanza kufungua mipaka

Lakini  wakati  baadhi  ya  magavana  wa  majimbo  ya  Marekani wakiweka  sasa  karantini  ya  siku  14  kw wasafiri  kutoka  katika majimbo  yaliyoathirika  zaidi, Umoja  wa  ulaya  umeanza  kufungua mipaka  yake. Wakaazi  wa  Marekani , Brazil  pamoja  na  Urusi iliyoathirika  zaidi  na  virusi  hivyo  bado wananyimwa  ruhusa  ya kuingia  katika  mataifa  ya  Ulaya.

Shirika  la  afya  ulimwenguni WHO limeonya siku  ya  Jumatano kuwa  janga  hilo linaongezeka, kwa  zaidi  ya  nusu  ya  maambukizi ya  dunia katika  muda  wa  nusu  ya  mwaka  katika  mwezi  Juni pekee. Na  wiki  iliyopita  imeshuhudia  viwango  vya  juu, wakati kesi zimefikia  160,000  katika  kila  siku  moja ," Mkuu  wa  WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus  alisema.

Idadi  ya  maambukizi  imekuwa  ikipanda  katika  mataifa  ya Amerika ya kusini . Brazil  ikiwa  na  uchumi  mkubwa  katika  eneo hilo, ina  karibu kesi milioni 1.5 zilizothibitishwa, ikiwa  ni  ya  pili  tu kutoka  Marekani.

Idadi  ya  maambukizi nchini  Ujerumani  imeongezeka  kwa  watu 446  na  kufikia  watu 195,674, data  kutoka  taasisi  ya  Robert Koch ya  magonjwa  ya  kuambukiza  zimeonesha  leo Ijumaa.

Korea  kusini imeripoti maambukizi  mapya  63 jana, wengi  wao ni kutoka  ndani  ya  nchi  hiyo nje ya mji  mkuu  Seoul, na  kusababisha kurejea  kwa  vizuwizi vikali vya kuzuwia  kusogeleana  wakati uwezekano  wa  wimbi  la  pili la  ugonjwa  huo likiwatia  wasi  wasi maafisa.