Jinsi ya kufanikiwa katika maisha

 

Mara nyingi maisha hutupeleka sehemu ambazo hatuzielewi, tunahangaika na tunashindwa kusonga mbele sababu ya kusahau vitu vidogo vidogo ambavyo ndivyo vinabeba muhimili unaoshikilia uwezo wetu wa kukua katika mafanikio, kiumeni.com imekuandalia ukumbusho wa kanuni zinazotufanya tufanikiwe na kutujenga katika mafanikio.
 
Wewe ni mtu pekee unaowajibika katika kutafuta na kujiletea mafanikio yako mwenyewe.
Sehemu bora na nzuri ya maisha yako itakuja pale utakapoamua na kujua hayo maisha ni maisha yako na hakuna mtu mwingine anayeweza kuyabadilisha tofauti na wewe mwenyewe, hakuna wa kumlilia, hakuna wa kumtegemea tofauti na kujitegemea mwenyewe, kutakua na hali ngumu zitakazo kusumbua ila ukiamini kwa moyo wako wote na kuongoza maisha yako utafanya kile ambacho hutaamini unaweza na utashangazwa na uwezo ulionao.

Usifate nani kafanya nini, unatakiwa ufanye maamuzi yako mwenyewe na kwa sheria ulizojitengenezea mwenyewe na mafanikio yatafuata, mwanzo hua ni mgumu na furaha sio kitu unachopaswa kuangalia kwa sasa, usikubali kuishi kwa kiwango cha maisha ulichonacho sasa, badili hali yako kwa kukataa na kuchukia mazingira uliyonayo sasa maana unaweza kuishi kwenye hali nzuri zaidi kuliko hii ukifanya maamuzi ya uhakika, na siku zote kumbuka mbuyu ulianza kama mchicha.

Siyo mpaka uvumbue dhahabu au kompyuta ndo ufanikiwe.
Kuwa na mafanikio hakuhitaji uvumbue kitu chochote, ukiwa na wazo jipya na fikra chanya zenye maono ya kugeuza sababu na athari kuwa wazo la kimaendeleo kwa kutumia mazingira yaliyopo inaweza kukusaidia sana, hata hivyo unaweza kuvumbua kitu na bado ikawa njia ngumu kupata mafanikio, ukiangalia watu wengi hasa waliopata mafanikio makubwa wengi wao waliendeleza vitu vilivyopo kwa kuvipatia muonekano mpya ambao ulikuwa haukufikiriwa hapo kabla au walitumia kitu hicho hicho kilichokuwepo na kukipa mguso wa kipekee wa kimasoko na kikawaletea mafanikio makubwa zaidi kwa kukiuza zaidi, ubunifu ni kuunganisha mambo, kuunganisha mambo ina maana ya kutafuta msukumo kutokana na mawazo makubwa ambayo tayari yapo na kuyafanya yawe na utofauti ambao mwanzo haukuonekana.

Hakuna maendeleo bila matendo.
Jambo ambalo hujalianzishwa leo haliwezi kamwe kufanikiwa kesho, mawazo mengi mazuri yameshindwa kufanikiwa kwa sababu wenye hayo mawazo wameshindwa kuyafanyia matendo, jambo moja kuu la kuweka maanani, mafanikio sio kitu cha kuonekana wakati bado hujafanya kitu, usitegemee kitu kikubwa wakati bado haujakifanyia tendo lolote, anza kwa kulitenda kwanza na kuwa na subira, ukishalianza hatua zinazofuata baada ya hapo zikiwa na nia na kutendwa katika hali sahihi mafanikio lazima yaonekane, kila kilichoanza kwa kutoonekana baada ya muda wa matendo lazima kianze kuonekana na chenyewe.

Uvumilivu hushinda.
Kama msemo wa kale unavyosema, "mvumilivu hula mbivu", maji ya mto hupasua jiwe si kutokana na nguvu na kasi ya maji, ila inatokana na ubishi na uvumilivu wa maji kupita sehemu ile ile, ukiwa mvumilivu hata kama umeanza kwa kukosea mwisho wa siku utafanikiwa kwa chochote unachofanya.

Kufeli sio tija ya kuacha kujaribu.
Usije amka miaka sabini na tano na ukaanza kuhesabu kile ambacho ungeweza kufanya ukiwa angali na nguvu za kukifanya, kama umeamua kufanya kitu bora ufanye na si kutoa visingizio na kutumia uoga wako kugeuza maamuzi yako mwenyewe, watu wachache sana hufanya kitu sahihi kwa mara ya kwanza ila huendelea kufanya wanachofanya mpaka hapo wanapokipatia, binadamu hawapai ila hutembea hatua moja baada ya nyingine na hufika waendapo na hata kimawazo pia hufanya hivyo hivyo na kutimiza malengo yao.

Kuwa makini na kila kitu.
Ukiwa umetingwa na mawazo ya kuangalia nyuma na pembeni kwa kile ambacho nafsi yako inahuzunika kwa kutokifanya na ukiangalia kwa umakini unajikuta hukufanya kwa sababu ya woga, huu ndio muda wa kukifanya hicho kitu, ila kuwa makini na ukifanyacho achana na hofu, hofu uliyonayo ndo itakufanya usikifanye vizuri, kama wasemavyo "kunguru muoga hukimbiza bawa lake".

Mawazo chanya huleta uzalishaji.
Mawazo ndo usukani uendeshao maisha yetu kuelekea uelekeo flani, iwapo mawazo yako yakiwa chanya basi na maisha yako pia yatakuwa endelevu na iwapo mawazo yakiwa tofauti, mawazo hasi basi ujue hapo maisha lazima yakushinde na kukuendea kombo, ndo maana kiumeni.com tunaamini mafanikio huanza kichwani kwa mawazo endelevu na hushuka moyoni kwa nia iliyo madhubuti.

Unatakiwa uwamini unaweza.
Jambo la kwanza na siri kubwa ya mafanikio ni kiasi gani unajiamini, mafanikio huanza na ndoto na ili matendo yazae matunda lazima ujiamini asilimia mia ya kuwa unaweza na kujua unachokifanya.

Kusaidia wengine ndo moja ya sehemu ya kuwa na mafanikio.

Watu waliofanikiwa daima huja na mawazo mapya na njia bora za kuwasaidia wengine, hii ikiwa na maana iwapo ukiweza kusaidia wengine, hayo hayo mawazo endelevu ndio yatakusaidia na wewe pia kukua katika mafanikio, mafanikio yako ya muda mrefu yanatokana na jinsi unavyonufaisha jamii ikuzungukayo.

Mafanikio ni safari ya hatua zisizohesabika.
Mafanikio ni ukuaji unaoendelea kutoka hatua moja hadi nyingine, hakuna mafanikio ya moja kwa moja, utatoka hatua moja na ukifika nyingine utaona njia nyingine tena ya kufanya mambo tofauti, kitu muhimu katika maisha siyo sehemu tulioifikia bali ni mwelekeo tunaokwenda.

Post a Comment

0 Comments