Wanajeshi wavamia ofisi za chama cha Bobi Wine


Msemaji wa chama cha upinzani nchini Uganda, National Unity Platform (NUP), amesema ofisi zao zimevamiwa na maafisa wa jeshi wakati ambapo maajenti wa chama hicho walikuwa wamekutana kuweka pamoja nyenzo zitakazotumika kupinga matokeo ya uchaguzi.

Akizungumza na BBC Newsday, Joel Ssenyonyi amesema chama hicho kilikuwa kwenye mchakato wa kukusanya fomu za matokeo ya uchaguzi zenye ushahidi wa wizi wa kura katika uchaguzi uliokamilika.

Bwana Ssenyonyi ameongeza, nyumba ya kiongozi wa chama hicho Bobi Wine bado imezingirwa na wanajeshi.

Rais Yoweri Museveni – ambaye ameshinda uchaguzi kwa muhula wa sita – amekanusha taarifa za wizi wa kura.

"Kila mgombea urais anakuwa na fomu ya kupinga matokeo, kwanini hataki tuwasilishe fomu hiyo tuliyopewa na tume ya uchaguzi?" Bwana Ssenyonyi ameuliza.

Upinzani pia umesema kwamba walikuwa na picha na video kama ushahidi wa kile walichokusanya.

"Bwana Museveni anajua kwamba tuna vitu hivyo ndio maana aliamua kufunga intaneti; hataki tuweke vitu hivyo wazi ili raia wote wa Uganda na jamii ya kimataifa waweze kufahamu jinsi alivyo mlaghai," amesema.

Intaneti imerudishwa nchini Uganda baada ya kuzimwa kwa muda wa siku tano, ingawa mitandao ya kijamii bado imefungwa na mtu anaweza kupata mawasiliano hayo kwa kutumia VPN.

Wakati huo huo, msemaji wa polisi nchini Uganda amezungumza na kituo cha habari cha NTV Uganda na kusema:

‘’Bobi Wine hajawekwa katika kifungo cha nyumbani, kuna uwepo wetu kwake nyumbani kwasababu chama cha NUP kilikuwa na mipango ya kusababisha vurugu.’’

Msemaji huyo Fred Enanga amethibitisha kwamba mawakili wa Bobi WIne wanaweza kuwasiliana na mteja wao.

Post a Comment

0 Comments