Urusi yaishambulia EU kwa kutangaza vikwazo kuhusu Navalny


Wizara ya Mambo ya Kigeni ya Urusi imeshutumu uamuzi wa Umoja wa Ulaya kuwawekea vikwazo maafisa wa Urusi kuhusiana na ukandamizaji unaofanywa dhidi ya mkosoaji wa serikali ya Urusi Alexei Navalny na wafuasi wake. 

Mawaziri wa Mambo ya Kigeni wa Umoja wa Ulaya mapema jana walikubaliana kuwawekea vikwazo maafisa wanne waandamizi wa Urusi, baada ya mawakili wa Navalny kuwahimiza mawaziri hao kuwalenga matajiri wanaotuhumiwa kuufadhili utawala wa Rais Valdmir Putin. 

Wanadiplomasia wa Ulaya hawakuwataja maafisa hao waliolengwa wala kutoa maelezo kuwahusu. Katika taarifa, wizara ya mambo ya kigeni ya Urusi imesema vikwazo hivyo vipya vinakatisha tamaa na kuwa viliandaliwa chini ya hoja isiyokuwa na msingi wowote. 

Awali, Umoja wa Ulaya uliiwekea vikwazo Urusi kuhusiana na tukio la kupewa sumu Navalny, ambaye kwa sasa yuko kizuizini, ukiwaweka maafisa sita wa Urusi kwenye orodha mbaya mwezi Oktoba.

Post a Comment

0 Comments