Marekani yakanusha ripoti za Iran kuwaachia Wamarekani wanne

 


Afisa mwandamizi wa Ikulu ya Marekani amekanusha ripoti kutoka Iran kuwa makubaliano yamefikiwa na Iran ya kuwachiwa huru kwa Wamarekani wanne wanaoshikiliwa nchini humo. 

Mkuu wa Utumishi Ron Klain ameiambia televisheni ya Marekani ya CBS kuwa hakuna makubaliano yaliyofikiwa kwa sasa, lakini wanafanya kila liwezekanalo kuhakikisha kuwa Wamarekani hao wanarejeshwa nyumbani. 

Matamshi hayo ya Klain yanafuatia ripoti za televisheni ya taifa ya Iran, ikinukuu "chanzo cha habari chenye ufahamu", kuwa upande wa Marekani umekubali kuruhusu dola bilioni 7 ambazo ni fedha za Iran zilizozuwiwa na kuwaachia Wairan wanne wanaotuhumiwa kwa kukwepa vikwazo vilivyowekwa, kwa kubadilishana na Wamarekani wanne wanaotuhumiwa kwa upelelezi. 

Televisheni hiyo ya taifa pia iliripoti kuwa Nazanin Zaghari-Ratcliffe, aliye na uraia wa Uingereza na Iran na ambaye anashikiliwa Iran tangu 2016, anaachiwa huru baada ya malipo ya deni la kijeshi. 

Maafisa wa Uingereza hata hivyo wamepuuza ripoti hiyo wakisema mazungumzo yanaendelea.


Post a Comment

0 Comments