Serikali yapiga marufuku wanafunzi wanaoanza darasa lwa kwanza kudaiwa vyeti vya awali

 


Serikali imekiri kutowekeza vya kutosha katika elimu ya awali, na hivyo imepiga marufuku wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza kudaiwa vyeti vya ngazi hiyo ya elimu.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi Ummy Mwalimu ametoa agizo hilo leo bungeni leo Mei 3,2021 ambapo amesema Serikali ipo kwenye mchakato wa kuboresha elimu ya awali.

Waziri ametoa kauli hiyo kufuatia swali la nyongeza la mbunge wa Viti Maalum, Mariam Kisangi aliyehoji ni kwa nini wanafunzi wanaoandikishwa kuanza darasa la kwanza hulazimishwa kuwa na vyeti vya kuhitimu elimu ya awali hasa katika Jiji la Dar es Salaam.

"Mheshimia Spika,naomba nitoe tamko la kisera hapa, ni marufuku wazazi kudaiwa vyeti vya awali kama kigezo cha kuandika watoto wao darasa la kwanza, sababu kubwa ni kwamba hatujawekeza vizuri katika elimu ya awali," amesema Ummy.

Waziri amesema kwa sasa Serikali inajipanga kuwekeza zaidi katika elimu ya awali ambako bado kuna matatizo kidogo.

Awali Naibu Waziri katika Wizara ya Tamisemi David Silinde alisema madai ya vyeti kwa wanafunzi wanaoandikishwa hudaiwa kwa shule binafsi lakini si utaratibu wa Serikali.

Post a Comment

0 Comments