DC Jerry Muro, Kenani watua rasmi Singida

MKUU wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge amewapokea rasmi wakuu wapya wa wilaya za Ikungi, Iramba na Mkalama kufuatia mabadiliko na teuzi mpya zilizofanywa  na Rais Samia Suluhu Hassan mwishoni mwa wiki.

Miongoni mwa wakuu hao wa wilaya walioripoti ni pamoja na Jerry Muro ambaye anakwenda kuhudumu wilaya ya Ikungi, Kenani Kihongosi Iramba na Sophia Kizigo wilaya ya Mkalama huku Mhandisi Pascas Muragili Singida Mjini na Rahabu Mwagisa, Manyoni wakiendelea na nafasi zao kutokana na kutoguswa na mabadiliko hayo.


Akizungumza wakati akiwakaribisha wakuu hao wa wilaya ofisini kwake Dkt. Mahenge aliwaomba kufanya kazi kwa ushirikiano kama timu.

“Nawaomba tushirikiane kwa kila jambo na kupeana taarifa kabla ya kufanya chochote katika wilaya zenu hasa hizi operesheni mbalimbali,” alisema Mahenge.

Aidha Mahenge aliwaomba wakuu hao wa wilaya kuongeza nguvu na ushirikiano kwa kutumia ujuzi wa kitaaluma na uzoefu walionao katika kuleta mapinduzi ya kiuchumi ndani ya mkoa wa Singida.

Alisema Rais Samia Suluhu Hassan amewaamini na kuwateua kushika nafasi hizo kwa lengo la kuwatumikia wananchi na si vinginevyo.


“Namshukuru Rais Samia kwa kuendelea kuniamini na kunileta Singida, sina wasiwasi sababu viongozi wote niliowakuta wana uzoefu wa kutosha  ninaahidi kutoa ushirikiano kwa mkuu wa mkoa na viongozi wenzangu wote kwa maendeleo ya wilaya ya Ikungi na Singida kwa ujumla,” alisema Muro.


Kwa upande wake, Kenani Kihongosi alisema yupo tayari kupokea maelekezo na kumsaidia kwa karibu mkuu wa mkoa na Rais, lakini aliahidi kushirikiana na kila mpenda maendeleo kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yake mapya.

 

Post a Comment

0 Comments