Dkt. Gwajima akutana na Wadau wa maendeleo wanaochangia mfuko wa Afya wa pamoja

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amekutana na wadau wa maendeleo wanaochangia mfuko wa afya wa Pamoja (Health Basket Fund) na kujadili utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo upande wa sekta ya afya na kuona namna ya kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya wadau hao na Wizara.

Waziri Gwajima ameainisha mafanikio ambayo yamepatikana katika hati ya makubaliano ya mwaka 2015 hadi 2021 ambapo ubora wa takwimu umeongezeka kwa asilimia 91.3 mwaka 2020 kutoka asilimia 75 mwaka 2017 huku vituo vya afya vilivyofanyiwa uhakiki na kupewa nyota za ubora tatu au Zaidi vimefikia asilimia 20 kutoka asilimia 2 mwaka 2016.


Katika upande wa uwajibikiaji, Waziri Gwajima amesema Halmashauri karibu zote zimekua na bodi za afya ikiwa ni asilimia 92.3 mwaka 2020 kutoka asilimia 77 mwaka 2015, zikiwa na lengo la kuangalia utekelezaji wa majukumu ya Halmashauri katika sekta ya afya.

Aidha, Waziri Gwajima ameelezea suala la ukarabati wa vituo vya afya ambapo katika kipindi cha mwaka 2017/18 vituo vilivyokarabatiwa ni 304 ambapo kati ya hivyo, vituo 223 vimekarabatiwa kwa fedha za Mfuko wa afya wa Pamoja.

Waziri Gwajima amewaomba wadau wengine waweze kujiunga katika mfuko wa afya wa Pamoja ili kuweza kusaidiana na Serikali katika kuboresha maeneo mbalimbali ya Sekta ya afya ambapo Serikali pia imeandaa mpango mkakati wa kuchangia huduma za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu na kwa wakati.

Mwisho, Waziri Gwajima amewashukuru wadau hao kuwepo katika mfuko toka mwaka 1999 na wameendelea kuchangia katika sekta ya afya kwa kufuata taratibu za Serikali na kuonesha manufaa makubwa katika kuboresha huduma za afya nchini huku akiwahakikishia mazingira ya uwekezaji Tanzania kuwa ni salama hususan katika eneo la afya na hivyo kuwataka wadau wengine kuendelea kujiunga.


Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel, Wakurugenzi wa idara mbalimbali za Wizara ya afya pamoja na Balozi wa Denmark Mhe. Mette Nørgaard Dissing-Spandet, Balozi wa Usiswi Mhe. Chassot Didier, Mkurugenzi wa KOICA Tanzania Kyucheol Eo, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland Chloë Horne na wawakilishi kutoka UNFPA, UNICEF na Ubalozi wa Canada.

 

Post a Comment

0 Comments