https://monetag.com/?ref_id=TTIb Kama unataka kuwa Mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, Acha kufanya mambo haya | Muungwana BLOG

Kama unataka kuwa Mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, Acha kufanya mambo haya

 

Mara nyingi huwa sio kitu kigeni kwa mtu ambaye ni  mjasiriamli wakati mwingine kufanya maamuzi yasiyo sahihi, kukosea hapa na pale na hata wakati mwingine kufanya biashara na watu ambao sio sahihi ambao wanauwezo wa kukurudisha nyuma, hii huwa inatokea sana bila kujua.

Hiyo yote inakuja kutuonyesha kuwa katika suala zima la ujasiriamali makosa huwa yapo na ni muhimu sana kuweza kutusaidia kusonga mbele pale tunapochukua jukumu la kujifunza kutokana na makosa. Hata hivyo huwa yapo makosa ambayo huwa tunaweza kuyaepuka ikiwa kweli tuna nia ya kuwa wajasiriamali wakubwa. Kama unataka kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, acha kufanya mambo haya:-

1. Acha kuogopa sana ushindani wa kibiashara.
Ili uwe mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, kitu pekee ambacho hutakiwi kuogopa sana ni ushindani wa kibiashara. Badala ya kuogopa ushindani kaa chini na kisha ujifunze ni kitu gani unachotakiwa ufanye katikati ya ushindani huo mkubwa unaouona. Kama una jiamini na bidhaa zako sokoni au biashara yako huna haja ya kuogopa sana upinzani. Wajasiamali wengi kuna wakati huwa ni waoga sana wa ushindani kiasi cha kwamba hutumia pesa na njia nyingine mbaya kukabiliana na upinzani. Badaa ya kuogopa upinzani, jifunze sana kutengeneza wateja wapya, kuboresha huduma zako na kila siku mafanikio utayaona katika biashara yako na utakuwa umefukia ushindani.

2. Acha kutaka kujihusisha na kila biashara.
Ni muhimu kuzingatia na kuweka nguvu zako zote hasa kwenye biashara yako hususani katika kipindi ambacho biashara yako haijakuwa sawasawa. Katika kipindi ambacho unaendeleza biashara yako ili ikue na kufikia viwangi vya juu unavyotaka acha kupenda kujihusisha na biashara nyingine ambazo zinaweza kukupunguzia nguvu kwenye biashara kubwa. Watu ama wajasiriamali ambao mara nyingi huwa ni watu wa tamaa kwa kutaka kila kinachopita mikononi mwao wakifanye. Hili ni jambo la hatari, kwa sababu mambo mengi hutaweza kufanikisha yote kwa pamoja.

3. Acha kuwa na malengo ya muda mrefu wakati wote katika biashara yako.
Katika biashara kuna wakati mambo huwa yanabadilika tena kwa kasi kubwa sana kuliko. Unapokuwa mjasiriamali  jukumu lako kubwa ni kuhakikisha unaifikisha biashara yako mahali ambapo ni salama hata kama kuna wakati mambo yanabadilika. Hii ikiwa na maana kuwa kuna wakati, inabidi ujifunze kutokufikiria sana biashara yako itakavyokuwa baadae na kujikuta umesahau majukumu yako ya sasa ya kuifanya biashara yako ili isimame na kusonga mbele. Kumbuka si maanishi usiwe na malengo ya muda mrefu katika biashara yako, ninacholenga hapa usifikirie muda wako wote kwa jisi biashara yako itakavyokuwa na kusahau sasa  hiyo ni hatari kwako.

4. Acha kuwa na makadirio makubwa ya faida.
Jukumu kubwa unalotakiwa kuwa nalo kama mjasiriamali ni kuhakikisha unakuza idadi ya wateja kwa jinsi unavyoweza hili ndilo jukumu lako kubwa. Acha kufikiria sana juu ya faida kubwa utakayopata kutokana na biashara hiyo unayoifanya. Kumbuka, kuwa huwezi ukapata faida yoyote ile kubwa kama una idadi ndogo ya wateja. Jifunze mbinu na namna jinsi ambavyo utakavyoweza kuwa na wateja wa kutosha katika biashara yako. Ukifanikiwa hili utaweza kupata faida kubwa sana ambayo unaifikiria uwe nayo katika biashara yako.

5. Acha kutegemea chanzo kimoja cha fedha.
Kama una lengo la kuwa mjasiriamali mkubwa katika maisha yako na hatimaye kuwa huru kifedha, acha kutegemea chanzo kimoja cha fedha. Kama utafanya biashara kwa kutegemea chanzo kimoja cha pesa elewa kabisa hutafika mbali sana kimafanikio kama unavyofikiri. Unapokuwa na vitega uchumi vingi hivi vitakusaidia kuongeza pato lako siku hadi siku na utajikuta mwisho wa siku una kiasi kikubwa cha pesa ulichokikusanya kwa matumizi ya leo na baadae. Wajasiriamali wote wenye mafanikio makubwa hawategemei chanzo kimoja cha pesa ni watu wenye vianzio vingi vya pesa. Kama na wewe unataka kuwa mjasiriamali wa mafanikio, jiwekee vyanzo vingi vya pesa. 

6. Acha kuwa na matumizi makubwa ya pesa.
Ni hatari sana kutaka kukua kibiashara huku ukiwa ni mtu wa matumizi makubwa ya pesa zako. Kama unataka kufika mbali kwenye safari yako ya ujasiriamali, futilia mbali matumizi mabovu ya pesa uliyonayo. Unapokuwa na matumizi mabovu ya pesa unakuwa kama hufanyi kitu, kwa sababu unakuwa unapoteza pesa nyingi sana ambayo ilikuwa haina sababu ya kupotea hata kidogo. Jifunze kutumia pesa zako vizuri na kwa utaratibu maalum unaoeleweka. Ili kufanikisha hili hakikisha unatengeneza bajeti yako,ambayo itakuwa inakuongoza.

Kwa kumaliza naomba niseme hivi, kuwa mjariamali mkubwa na mwenye mafanikio unahitaji kujitoa kikamilifu na wakati mwingine kujikana kabisa na kuachana na hofu yakukabiliana na mambo.

Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya kibiashara na ujasiriamali kwa ujumla iwe ya mafanikio.

Post a Comment

0 Comments