Mahakama Kuu ya Tanzania imetupilia mbali kesi ya kikatiba ya kupinga kuhojiwa aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka kwa tuhuma za kuliita Bunge la Tanzania dhaifu.
Uamuzi huo umetolewa na jopo la majaji
watatu wa mahakama hiyo, lililooongozwa na Jaji Dk Benhajj Masoud,
akishirikiana na majaji Elinaza Luvanda na Yose Mlyambina.
Katika
uamuzi huo ulioandikwa na Jaji Luvanda kwa niaba ya jopo hilo, wa
Oktoba 7, mwaka huu ambao Mwananchi limeuona nakala yake leo Jumatatu,
Oktoba 25, 2021, mahakama hiyo imeitupilia mbali kesi hiyo ikisema kuwa
haina mashiko ya kisheria na kwamba mdai hakuwa na hoja za msingi.
Shauri hilo la maombi mchanganyiko namba 01 la mwaka 2019, lilifunguliwa na Kiongozi wa Chama cha Alliance for Change and Transparency (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe Mahakama Kuu, Masjala Kuu, dhidi ya Spika wa Bunge, Job Ndugai na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Katika
shauri hilo Zitto alikuwa akipinga uamuzi wa Spika Ndugai kumtaka, CAG
Profesa Assad kufika mbele ya kamati hiyo kuhojiwa kutokana na kauli
yake aliyoitoa wakati akihojiwa na Redio ya Umoja wa Mataifa, nchini
Marekani Januari 7, 2019, kuwa Bunge la Tanzania ni dhaifu.
Zitto
ambaye alikuwa akiwakilishwa na wakili wa kujitegemea Jebra Kambole
alikuwa akidai kuwa kitendo cha Spika kumuita CAG kuhojiwa kwenye kamati
ya Bunge kwa kauli hiyo hakikuwa halali na kwamba kilikuwa kinyume cha
Katiba.
Wakati wa usikilizwaji wa shauri hilo wakili wa Zitto,
Kambole alidai kuwa CAG alikuwa akitoa maoni yake kuhusiana na majukumu
yake kama CAG nchini Tanzania na kwamba alikuwa akitumia uhuru wake wa
kujieleza unaolindwa na Katiba ya nchi na mikataba ya Kimataifa.
Alisisitiza kuwa mamlaka hayo ya Bunge kumuita mtu yeyote chini ya Sheria ya Kinga, Madaraka na Haki ya Bunge yana ukomo kwa kuwa kuna baadhi ya watu wana kinga ya kisheria, akiwemo CAG ambaye alidai kuwa halazimiki kutimiza maelekezo ya mtu au idara yoyote ya Serikali.
Badala yake
wakili Kambole alidai kuwa taasisi yenye mamlaka pekee ya kuhoji jambo
lolote linalofanywa na CAG ni Mahakama na si Kamati ya Bunge.
Mahakama katika uamuzi baada ya kurejea Sheria na Kanuni za Bunge nayo imekubalinana na hoja za Serikali kupitia kwa Wakili Mkuu wa Serikali (Solicitor General-SG), Gabriel Malata ikisema kuwa Bunge au Kamati ya Bunge ina mamlaka ya kumtaka mtu yeyote kufika mbele yake.
“Ni
kweli kwamba CAG analindwa chini ya masharti ya Ibara ya 143(6) ya
Katiba. Hata hivyo haki hiyo hapa ina mpaka kwa kumlinda CAG wakati tu
anatekeleza majukumu yake.” imesema mahakama hiyo katika uamuzi huo, kwa
tafsiri isiyo rasmi na kunukuu Ibara hiyo ndogo ya 6 ya Ibara ya 143 ya
Katiba.
Mahakama hiyo imesema kuwa ingekubali kuwa CAG
alikuwa anatoa maoni yake katika dhana ya uhuru wa kujieleza, lakini
ikasema kuwa kipimo cha hilo ni kama kauli hiyo aliyoitoa wakati wa
mahojiano hayo ilikuwa inahusiana na utendaji kazi wake kama CAG nchini
Tanzania.
“Tunafahamu kwamba mahojiano yalihusiana na taarifa
za CAG na mapendekezo yanayotolewa humo. Lakini hakuna mahali popote
paliposemwa kwamba madai ya udhaifu wa Bunge ni miongoni mwa mapendekezo
yake, ili kuwa na haki hiyo.” imesema mahakama hiyo.
Imesema
kuwa kama taarifa ya CAG ingekuwa na maoni hayo miongoni mwa mengine
kuwa Bunge ni dhaifu, basi kauli ya CAG ingekuwa imelindwa na Ibara ya
143 (6) ya Katiba.
0 Comments