Waziri Dkt. Kijaji avitaka vyombo vya habari kutangaza sherehe za miaka 60 ya Uhuru

Waziri wa Habari, Mwasiliano na Teknolojia  ya Habari, Dkt. Ashatu Kijaji amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na kufanya kazi na vyombo vya habari katika kutangaza  mambo mbalimbali yanayofanywa na Serikali kwa watanzania.

Akizungumza katika Mkutano wake na Wahariri wa Vyombo vya Habari nchini, Waziri Dkt.  Kijaji amesema lengo la Serikali ni kujenga uimara wa vyombo hivyo ili viweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuwaelimisha, kuburudisha na kutangaza mandeleo ya nchi kwa wananchi.

“Ndugu Wahariri lengo la Mkutano huu  ni kujitambulisha kwenu kwani tangu niteuliwe, Jambo hili ni muhimu hususan baada ya Mhe. Rais kuamua kwamba tasnia ya Habari sasa isimamiwe na Wizara yangu na kuunda Wizara Mpya yaani Wizara ya Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari, kwa hiyo ndugu wahariri ninaomba ushirikiano katika kukuza hii tasnia”, Alisema Dkt. Kijaji.

 Dkt Kijaji alisema kuwa ushirikiano wa Vyombo vya Habari na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ni  tunatimiza takwa la kisheria   Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inatamka kuwa kila mtu yuko huru kutoa  maoni na kutoa mawazo yake,  kutafuta, kupokea na kutoa habari kupitia chombo chochote bila ya kujali mipaka ya nchi.

Aidha Dkt. Kijaji alivishukuru Vyombo vya Habari nchini kwa kuendelea kuelimisha na kutoa  ushirikiano katika changamoto kubwa ya UVIKO 19, ambapo aliwataka waendelee kufanya kazi kwa weledi ili wananchi wapate elimu na kuchukua maamuzi sahihi ya kuchanja na kujikinga na madhara ya janga hilo.

Katika hatua nyingine Dkt. Kijaji alisema kuwa ushirikiano wa Vyombo vya habari na Serikali kupitia Wizara yake ni moja na nguzo muhimu katika kuendeleza sekta hiyo kwani ni sekta ambayo kwa kiasi kikubwa ndiyo inafanya wananchi kupata taarifa ya utekelezaji wa miradi na mambo mbalimbali ya Serikali, lakini pia inaonyesha wadau wa maendeleo nini Serikali inafanya.

 “Pamoja na juhudi kubwa mnayoifanya, naendelea kuwaomba ushirikiano mkubwa kutoka kwenu ili tuweze kuindeleza sekta ya habari hapa nchini na kutangaza masuala muhimu na mazuri yanayofanywa na Nchi yetu ikiwa ni pamoja na miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali, Wadau wa Maendelo na Wananchi wetu kwa ujumla wao”Alisema Dkt Kijaji.

Kuelekea Maadhimisho ya Miaka 60 ya Uhuru, Dkt. Kijaji alieleza umuhimu wa vyombo vya Habari katika kuelezea nchi ilikotoka, ilipo na inapokwenda, ambapo kuelekea siku hiyo ya  tarehe 9 Disemba 2021, vyombo vya habari vinatakiwa kueleza maendeleo na mambo mbalimbali yaliyofanyika tangu uhuru

Aliongeza kuwa kutokana na umuhimu wa sherehe hizo, Watanzania wote hawana budi  kujivunia miaka 60 ya Uhuru  wakiwa na amani na maendeleo katika  sekta mbalimbali ikiwepo tasnia ya habari.

“Naomba nitumie fursa hii kuwaomba wanatasnia ya habari kushiriki kikamilifu katika kutangaza shughuli zote zinazohusu Uhuru wa nchi yetu kama sehemu muhimu ya kutoa elimu kwa Watanzania na dunia kwa ujumla. Umoja wetu katika jambo hili utasaidia sana kuelimisha wananchi”, Alisema Dkt. Kijaji.

Akijibu Swali lililoibuliwa na Wahariri, kuhusu Maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, Dkt. Kijaji alisema kuwa maagizo yote yaliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu kufunguliwa kwa media mbalimbali zikiwemo zile za magazeti na online za Wizara inalifanyia kazi agizo hilo na atahakikisha anapata ufumbuzi hivi punde.


Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Zainabu Chaula amevitaka vyombo vya Habari kufanya kazi kwa weledi na kwa kufuata sheria kwani kwa kufanya hivyo tasnia itakua na kuwa na watalaam zaidi.

“ Waandishi wa Habari, tukifanya kazi kwa weledi hakuna kuvutana na fujo haziwezi kutokea, tukifanya kazi zinazotuhusu hakuna vurugu yeyote kwa hiyo tufanye kazi kwa kufuata sheria na kutumia taarifa vizuri ili kutoa taarifa za kuaminika”,
 

Post a Comment

0 Comments