Dkt Gwajima akagua mradi wa Hospital singida

 


Katika kuimarisha miundombinu ya matibabu ya huduma za kibingwa Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inatekeleza mradi wa ujenzi wa majengo mapya ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ambapo tayari imeshatoa shilingi bilioni 5.9 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo kubwa la ghorofa tatu. Jengo hili litatoa huduma za maabara, upasuaji na wodi za kulaza wagonjwa mbalimbali. ili kukamilisha majengo yote zinahitajika jumla bilioni 13.5.


Kwa upande mwingi serikali pia inatekeleza miradi ya maendeleo na mapambano dhidi ya UVIKO 19 ambapo kwa hospitali ya rufaa ya mkoa wa singida zimetengwa jumla shilingi bilioni 5.8 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la huduma kwa wagonjwa wa dharura na mahtuti, na vifaa vyake, kununua CT scan, Xray, nyumba ya mtumishi na kuimarisha mifumo ya matibabu kupitia teknolojia ya kidigitai (telemedicine) jambo litakalopunguza uhaba wa wataalamu na kuharakisha matibabu.


Amebainisha hayo Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Dkt Dorothy Gwajima katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jamii ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya Afya na kukagua utoaji huduma kwa wananchi.


Mkuu wa Wilaya ya Singida Pasacas Buragiri akimuwakilisha Mkuu wa mkoa amemhakilishoa Waziri wa Afya Dkt Gwajima kwamba serikali ya wilaya na mkoa imejipanga kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo kwa lengo la kutekeleza maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amebaini changamoto za wananchi wa singida ambao miaka mingi wanakabiliwa wa ukosefu wa hospitali ya wilaya na hospitali nzuri ya kibingwa ambayo ikikamilika itasaidia kuhamisha hospitali ya mkoa na majengo yake kutumika kuwa hospitali ya wilaya ili wananchi wa mji wa Singida wapate huduma kwenye Maeneo yao.


Wakati huo huo Dkt Gwajima ametembelea hospitali Teule ya Makiungu iliyojengwa mwaka 1954 na wamisionari ambao walikabidhi hospitali hiyo kwa masista wa kanisa katoliki kwa lengo la kutoa huduma ya afya kwa wakina mama sajawazito wakati wa kujifungua ili kulinda usalama wa maisha ya mama na mtoto.


Katika ziara yake Dkt Gwajima ameshuhudia uwekezaji mkubwa katika sekta ya Afya kwa kujenga Hospitali itakayotoa matibabu ya kibingwa inayogharimu kiasi cha shilingi Bilioni 10 kwa lengo la kuunga mkono juhudi za Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan aliyepania kufanya mapinduzi makubwa sekta ya Afya hapa nchini


Dkt Gwajima amesema uwekezaji  huo utaleta chachu ya maendeleo kwa jamii kupata huduma kwenye maeneo yao ili kupunguza adha kwa wananchi kufuata huduma umbali mrefu pia Hospitali hiyo ya kibingwa yenye vifaa tiba vya kisasa MRI na CT Scan itasaidia Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa wote hali itakayoipunguzia serikali gharama, changamoto na malalamimo kwa kuwa na mwelekeo thabiti wa huduma bora za Afya.


Post a Comment

0 Comments