https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mahakama yamsafisha askofu kwa mashtaka ya ubakaji wa mtawa, India | Muungwana BLOG

Mahakama yamsafisha askofu kwa mashtaka ya ubakaji wa mtawa, India


Mahakama ya India imemuondolea mashtaka askofu mmoja aliyeshtakiwa kwa kumbaka mtawa mmoja kati ya mwaka wa 2014 na 2016 katika kesi ambayo ilishtua jumuiya kongwe za Kikristo nchini humo.


Franco Mulakkal, mwenye umri wa miaka 54, alikamatwa kutoka jimbo la kusini la Kerala mwaka wa 2018.


Alikuwa amekanusha madai hayo.


Kesi hiyo ilizua maandamano makubwa baada ya mtawa huyo kudai kuwa Kanisa Katoliki lilipuuza malalamishi yake.


Vatikani ilikuwa imemwondolea askofu kazi zake kwa muda.


Siku ya Ijumaa, mahakama ya mjini Kottayam ya Kerala ilimkuta hana hatia ya mashtaka. "Upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashtaka yote dhidi ya mshtakiwa," alisema Jaji wa vikao vya ziada vya Kottayam (ASJ) G Gopakumar.


Mawakili wa mtawa huyo walisema watapinga uamuzi huo katika mahakama kuu.


Lakini timu ya wanasheria ya askofu huyo ilisema "imesambaratisha ushahidi wote" dhidi yake. "


Ni kesi yenye changamoto kubwa. Ni lazima ipelekwe kwenye mahakama kuu. Ni sawa," Raman Pillai, ambaye aliongoza timu ya utetezi ya Bw Mulakkal, aliambia BBC Hindi.


"Lakini mahakama ilisema hakuwa na hatia. Ni wazi, ushahidi ambao ulitolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka ulitupiliwa mbali. Hii ina maana kwamba shtaka lilikuwa la uongo. Hakukuwa na ubakaji hata kidogo," aliongeza.


Bw Mulakkal alikuwa askofu wa dayosisi ya Jalandhar katika jimbo la kaskazini la Punjab.


Mshitaki wake ni wa Wamisionari wa Yesu, huko Kerala ambalo ni sehemu ya dayosisi ya Jalandhar. Alidai kuwa askofu huyo alimbaka mara 13 na mashambulizi hayo yalitokea alipotembelea nyumba ya watawa alikokuwa akiishi katika jiji la Kottayam, Kerala.

Post a Comment

0 Comments