https://monetag.com/?ref_id=TTIb Meli ya kwanza ya nafaka kwelekea Afrika kutoka Ukraine yaanza kupakiwa | Muungwana BLOG

Meli ya kwanza ya nafaka kwelekea Afrika kutoka Ukraine yaanza kupakiwa


Meli ya kwanza ya nafaka inayoelekea barani Afrika kutoka nchini Ukraine tangu uvamizi wa Russia mwezi Februari mwaka huu ilitia nanga katika bandari ya Pivdennyi, jana Ijumaa, waziri wa miundombinu wa Ukraine alisema.


"Meli ya mizigo iitwayo MV Brave Commander iliwasili katika Bandari ya Bahari ya Pivdennyi, na hivi karibuni nafaka kutoka Ukraine itawasilishwa Ethiopia," Waziri Oleksandr Kubra-kov aliandika kwenye Twitter.


Baada ya kupakiwa, MV Brave Commander itabeba shehena ya nafaka za Ukraine chini ya Mpango wa Chakula Duniani, WFP, hadi Ethiopia kupitia bahari ya Black Sea.


Mpango huo ulipitishwa na Umoja wa Mataifa kwa ushirikiano na Uturuki mwishoni mwa Julai.


Kwa miezi kadhaa sasa, vita vya Russia nchini Ukraine vimesababisha uhaba wa chakula katika maeneo mengi kote duniani kutokana na kufungwa kwa baadhi ya njia na kuharibiwa kwa miundombinu huku baadhi ya mataifa yakiilaumu Russia kwa mgogoro huo.


Safari ya kwanza tangu Russia walipoivamia Ukraine na kuzuia usafirishaji kupitia Black Sea miezi mitano iliyopita ilifanyika Agosti Mosi mwaka huu, huku waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine akiiita “siku ya nafuu kwa dunia,” hasa kwa nchi zilizotishiwa na uhaba wa chakula na njaa kwa sababu ya kuvurugika kwa usafirishaji wa nafaka.


Safari hizi zimewezekana baada ya Uturuki na Umoja wa Mataifa kusimamia makubaliano ya kusafirisha nafaka na mbolea kati ya Russia na Ukraine mwezi uliopita katika makubaliano nadra ya kidiplomasia kwenye mzozo ambao unaendelea huku kukiwa hakuna suluhu katika eneo la tukio.


Inategemewa kwamba makubaliano hayo yatarahisisha mzozo wa chakula duniani na kupunguza gharama za nafaka.

Post a Comment

0 Comments