Kocha Msaidizi wa Azam FC, Idd Nassoro Cheche
Kocha Msaidizi wa Azam FC Idd Nassoro Cheche, amezidi kutamba mara baada ya kuiongoza timu yake kuichapa Simba mwishoni mwa wiki, ambapo amesema kuwa timu hiyo ya Simba ni kama mgonjwa wao ambaye tayari dawa yake walishaijua.
“Simba tayari tulicheza nayo mwanzo haijabadilika sana, mfumo wao waliocheza Unguja ndio ule ule ni sawa sawa na mgonjwa uliyeanza kumtibia umempa dawa karudi tena kwako unajua utampa dawa gani na matibabu yaendelee,” alisema.
Akizungumzia mchezo huo wa Jumamosi ambao bado umeacha kumbukumbu mbaya vichwani mwa mashabiki wa Simba, alisema kuwa wekundu hao waliingia kwenye mchezo huo wakitaka kujikomboa na ndiyo maana ilikuwa ngumu kwao kupata bao kipindi cha kwanza.
“Mimi namshukuru Mungu, nilisema mwanzo huko nyuma kuwa tunataka kuirudisha Azam FC yetu ambayo watu walikuwa wakiijua hapa kati tulipotea ni sehemu ya maisha kuna wakati unayumba, lakini sasa hivi tumeshaona wapi nini tufanye wapi tuelekee ili kuwarudishia ile hamu wachezaji watu na kufanya vizuri,” alisema.
Mara baada ya mchezo huo, Azam FC imefikisha jumla ya pointi 34 na kupanda hadi nafasi ya tatu ikilingana na Kagera Sugar lakini inaizidi kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa (GD), pia kwa sasa imebakisha pengo la pointi 12 kuifikia Yanga iliyo kileleni na 11 Simba iliyonafasi ya pili.
