Haya ndio malengo ya Simba kwa msimu ujao

Klabu ya Simba imesema kuwa malengo makubwa kwa msimu ujao ni kuleta ushindani mkubwa utakaoifanya klabu kuwa ndani ya timu tano kubwa barani Afrika.

Simba leo wana semina ya ndani ya wachezaji wa Simba pamoja na benchi la ufundi inayofanyika ilipo kambi yao iliyopo kwenye fukwe za Bahari ya Hindi ambayo inahusu historia ya klabu, kanuni, maadili, desturi, malengo ya mwaka 2019-20 na nidhamu.

Mulami Nghambi ambaye ni mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ndani ya Simba amesema kuwa "Tunataka kuwa moja ya timu tano bora Afrika na ili kufika huko kuna mambo mengi yanahitajika kufanyika," amesema.

Beki wa Simba, Gadiel Michael ambaye amesaini kandarasi ya miaka miwili akitokea Yanga amesema kuwa kazi kubwa kwa wachezaji ni kushirikiana kutafuta mafanikio.