Kanuni za kufanya kilimo bora

Kwa kilimo chochote kile ambacho unatamani sana kukifanya zipo kanuni na taratibu zake za kuweza kufanya hivyo. Baadhi ya mambo ya msingi ambayo ni muhimu kuweza kufanya hivyo ni pamoja na;

Kutayarisha shamba mapema
Shamba ni lazima litayarishwe mapema. Matayarisho hayo ni pamoja na kufyeka, kukwatua na kulima.

Kutumia mbolea: 
SAMADI: Ihamishiwe shambani mapema kabla ya mvua kuanza.
MBOLEA ZA VIWANDANI: Tumia mbolea za kupandia kama vile Minjingu Rock Phosphate (MRP), DAP na NPK. Zikifuatiwa na za kukuzia kama UREA na CAN.

Upanda  mapema
Panda mara mvua za kwanza zinapoanza kunyesha.

Kutayarisha mbegu bora mapema
Nunua mbegu au tayarisha mbegu nzuri kutokana na mavuno yaliyopita kama ulitumia mbegu mchanganyiko.

Mbegu chotara (hybrid) zisirudiwe. Mbegu bora ziwe zilizopendekezwa kwenye ukanda/eneo lako.

Panda kwa nafasi zinazotakiwa
Hakikisha umepanda kila zao kwa nafasi maalum inayoshauriwa kitaalam. Rudishia mapema pale ambapo mbegu hazikuota.

Kupalilia vizuri na kwa wakati
Hakikisha shamba lako halina magugu wakati wote kwa kupalilia mapema. Wakati wa kupalilia punguzia miche na kuinulia matuta.

Kudhibiti magonjwa, wadudu na ndege waharibifu wa mazao
Tumia njia za kitaalam za kudhibiti magonjwa, wadudu na ndege waharibifu wa mazao.

Kuvuna mapema
Vuna mazao yako mapema mara yanapokomaa na kukauka vizuri. Vuna kwa wakati ili kuepuka mazao yako yasiharibike kwa jua, mvua na wadudu.

Kuhifadhi mazao vizuri
Mara baada ya kuvuna na kukausha mazao vyema, hifadhi kwenye vyombo vya kuhifadhia kama vile vihenge na magunia. Hakikisha umeweka dawa za kudhibiti wadudu waharibifu.

Kusafisha shamba mapema baada ya kuvuna.
Ng'oa mabua na masalia ya mazao na kuyalaza kati ya matuta na kuyafunika kwa udongo ili yaoze mapema. Kwa mazao ya tumbaku na pamba ng'oa na kuchoma moto mabua yake mapema.