''Wapinzani wapigwe nondo''


Mjumbe wa halmashauri kuu wa Chama cha Mapinduzi CCM taifa, Musa Mwakitinya amewataka wanachama wa chama cha hicho nchini, kuwapa elimu ya kutosha wapinzani juu ya miradi na kazi zinazofanywa na rais kupitia serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuliko kuendelea kuwaacha wakiichafua serikali na chama hicho.

Ameyasema hayo mkoani Njombe wakati akizindua Njombe ya kijani pamoja na mbio za balozi kwanza kwa vijana wa chama hicho UVCCM mkoa wa Njombe watakao kimbia mkoa mzima kueleza utekelezaji wa ilani ya chama hicho.

“Tusipohubiri kazi alizofanya Mh.Rais hakuna watakaomsemea,sasa wale wengine huwa wanapita kuharibu na maneno machafu ya hovyo juu ya kazi zinazofanywa na Rais,tunahitaji kuwa wakalimani wengine hawawezi kuona wamejitia upofu,wamejitia uziwi hawaoni hizi kazi kama ujenzi wa mahospitali,kwa hiyo twendeni tuwachape vibao vya sera tuwaeleze mbona haya yanafanyika hamyaoni,na tukifanya hivi na uhakika moja kwa moja tutawazibua maskio yao na macho yao na wenyewe watayazungumza yale ambayo Rais amekuwa akiyafanya”alisema Mwakitinya

Aidha ameongeza kuwa “Tuna kazi kubwa ya kuelimisha watu,ukiona haelimiki mpige nondo zilizo nzito mpige hoja zilizo nzito,katika siasa tunazo lugha zetu ukizizungumza mwingine anaweza akateseka,lakini tukizungumza chama cha mapinduzi maneno haya kwa wapinzani inakuwa ni nogwa”aliongeza Mwakitinya

Kwa upande wake katibu wa umoja wa vijana UVCCM mkoa wa Njombe Amos Kusakula amesema tukio lililozinduliwa ni la umoja wa vijana kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu kwa lengo la kuwaeleza wananchi utekelezaji wa ilani ya chama cha mapainduzi kwa mwaka 2015-2020.

“kampeni hii lengo lake ni kueneza mafanikio na utekelezaji wa ilani ya chama cha mapinduzi kwa kutangaza miradi yote iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa mkoani Njombe na nchi kwa ujumla kwa kuwa wana CCM tunajua Rais amefanya nini sasa tuwakumbushe zaidi wanachama na wananchi wa kawaida”alisema kusakula

Baadhi ya wajumbe waliohudhulia katika mkutano huo wametoa baraka kwa vijana wao huku wakitoa wito kutumia lugha nyepesi kwa wananchi wanaokwenda kukutana vijijini.

Vijana 14 wa chama hicho mkoa wa Njombe wamekabidhiwa mabango yenye picha mbali mbali za miradi iliyotekelezwa na serikali ,picha ya Rais,bendera ya chama pamoja na bendera ya Rais kwa ajili ya kukimbia majimbo 6 ya uchaguzi mkoani humo ili kufikisha ujumbe huo.