Ijue mbolea itokanayo na magugu maji


Hii ni aina ya mbolea ya asili isiyokuwa na madhara yoyote kwa binadamu na wanyama. Mbolea hii hutengenezwa kwa kuvundika mimea ya baharini au maotea ya majini. Aina hii ya mbolea inafaa kutumika kwa kuchanganya na viua wadudu vyovyote ambavyo ni asidi au basic kwani utendaji kazi wake hauwezi kupote endapo itachanganywa.

Viambata vya mbolea

Mbolea hii ina vichocheo vya mimea ambavyo ni vya asili kama Auxins,  Cytokins na Gibberellins ambavyo hivi ni homoni za mimea ya asili yenye uwezo mkubwa wa kufanya mazao yaweze kumea vizuri na hatimaye kutoa mavuno mazuri Mbolea hii pia ina madini zaidi ya sabini ambayo yana uwezo mkubwa wa kustawisha na kuimarisha mazao kwa kiwango cha juu.

Kazi za mbolea hii:

1. Inaongeza uwezo wa mmea kuweza kufyonza madini na virutubisho mbali mbali kutoka kwenye udongo na pia kutoa mizizi kwa haraka.

2. Mbolea hii pia inaongeza uwezo wa mimea kujitengenezea chakula chake yenyewe.

3. Ina uwezo wa kusaidia uhifadhi wa unyevu nyevu katika udongo kwa muda mrefu.

4. Inafanya mmea uweze kuhimili hali ya ukame, ubaridi pamoja na magonjwa mbalimbali.

5. Inafanya mmea uweze kuota mapema kuongeza wingi wa mizizi na mimea kuwa na afya

6. Inaongeza kiwango cha mavuno ya mazao yako.

7. Inaongeza muda wa matunda au mazao kukaa muda mrefu baada ya mavuno kama ikitumiwa siku kumi kabla ya kuvuna.

Mimea ambayo inastahili mbolea hii
Mbolea hii inaweza kutumika katika mimea au mazao mbalimbali kwa mfano matunda yoyote, mboga za majani, mazao ya nafaka, dawa za mitishamba, maua, nyasi, pamba, nyanya, hoho, bilinganya, vitunguu, nk.

Pamba
Unaweza kutumia kuloweka mbegu zako kabla ya kupanda kwa kuchukua kiasi cha mililita 40 za bioplus na kuweka kwenye lita 20 za maji kisha kuloweka mbegu zako kwa masaa 5 hadi 10 ndipo uzitoe tayari kwa kupandwa. Inashauriwa kutumia kiwango cha mbolea cha mililita 60 hadi 90 kwa ekari moja. Wakati wa kutoa maua unashariwa kutumia kiwango cha mililita 180 kwa hekari moja. Kwa mara moja, changanya mililita 13 - 20 za mbolea kwenye lita 20 za maji na kisha nyunyizia kwenye mazao.

Mpunga
Kwa kuloweka mbegu, chukua mililita 60-90 za mbolea ya bioplus kisha changanya kwenye lita ishirini za maji na weka mbegu zako kwenye maji masaa manane mpaka kumi ndipo uzitoe tayari kwa kupandwa. Hiki kiwango unaweza kubadili kulingana na lita za maji unazotumia hivyo unaweza kutafuta ni kiasi gani cha dawa unachohitaji kuchanganya kwenye maji. Baada ya kuanza kutoa maua, chukua mililita 13-20 kisha weka kwenye maji ya lita 20 na nyunyuzia kwenye mazao. Hakikisha kuwa hekari moja hauzidishi kiasi cha mbolea chenye wingi wa mililita 240 kwa ekari moja.

Mahindi
Kwa kuloweka mbegu, chukua kiasi cha mililita 40 za bioplus na changanya kwenye maji lita 20. Weka mbegu zako ndani ya mbolea kwa masaa 8-10. Mahindi yakishatoa majani na maua, Chukua mililita 20 za mbolea kisha weka kwenye maji lita 20 na nyunyuzia mahindi. Hakikisha huzidishi kiwango hiki, na tumia mililita 720 za mbolea kwa ekari moja.

Mboga za majani
Chukua mililita 40 za mbolea kasha weka kwenye lita 20 za maji na nyunyuzia mboga. Unashauriwa usizidishe 720 mls za mbolea kwa hekari moja na unaweza kunyunyuzia mara tatu kwa kipindi chote cha zao kuwa shambani.

Matango, tikiti na nyanya
Chukua mililita 20 za mbolea kasha changanya na lita 20 za maji na nyuny-uzia kwenye mazao yako. Unashauriwa usizidishe kiasi cha 720mls kwa kila ekari kila unaponyunyuzia hii mbolea, na waweza kunyunyuzia hadi mara tatu mpaka kufikia mazao yako kuvuna. Pia unaweza kuitumia mbolea hii kwa mazao mengine kama matufaha, ndizi, maembe, soya nk.