Mwanamuziki nyota nchini Rwanda ashikiliwa na vyombo vya usalama

Idara ya upelelezi ya Rwanda imesema inamshikilia mwanamuziki Kizito Mihigo baada ya kufikishwa kwenye idara hiyo na polisi tarehe 12 mwezi Februari .

Kwenye ukurasa wa Twitter idara hiyo ya uchunguzi imesema Kizito anashutumiwa kujaribu kuvuka mpaka kwenda Burundi kinyume cha sheria kwa lengo la kujiunga na makundi ya wanamgambo wanaoipinga serikali ya Rwanda.Pia anashutumiwa kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Mamlaka ya uchunguzi imesema uchunguzi bado unaendelea kuhusu tuhuma zinazomkabili ili kufungua kesi dhidi yake.

Awali mwanamuziki huyo alidaiwa kutoweka hapo jana tangu alipozuiwa na wananchi Kusini Magharibi akidaiwa kujaribu kuvuka mpaka kuingia Burundi.

Mwanaume mmoja katika eneo la Nyaruguru ambaye alimuona mwanamuziki huyo jana, aliiambia BBC idhaa ya maziwa makuu kuwa alionekana kama mtu aliyetoka kwenye safari ndefu akiwa na begi zito na akiambatana na wanaume wawili.

Picha za mwanamuziki huyo nyota zilisambaa kwenye mitandao ya kijamii jioni.

''Nilikuwa hapo nilimuona, wanakijiji waliomzuia walisema alikuwa akijaribu kuvuka mpaka kwenda Burundi kwa kutumia njia za panya, kutoka hapa mpaka mpakani ni mwendo wa chini ya dakika tano''. Alisema.

Bwana Kizito na wanaume wawili walikabidhiwa kwa wanajeshi na polisi walioitwa na wanakijiji.

Polisi nchini Rwanda awali waliiambia BBC kuwa hawana taarifa bado kuhusu kukamatwa kwa mwanamuziki huyo.

Mwaka 2015, Bwana Kizito alikutwa na hatia kwa kosa la jaribio la kutaka kumuua Rais Paul Kagame na kuhamasisha vurugu dhidi ya serikali: alihukumiwa kifungo cha miaka 10 gerezani.

Mwezi Septemba mwaka 2018 aliachiwa huru kwa msamaha wa rais kwa sharti la kuwa atatoka nje ya Rwanda kwa ruhusa ya mahakama ya nchi hiyo.

Hatahivyo, alizuiwa ndani ya nchi, marafiki zake walithibitisha kuwa haonekani popote hii leo.

Raia wa Rwanda walikuwa wanasubiri mamlaka ithibitishe kukamatwa kwake na mashtaka yanayomkabili, au kuonekana bila kuwa na mashtaka.