Mwanamke mmoja mzee mwenye miaka 68 nchini Nigeria amejifungua watoto pacha na kuwaacha wengi na mshangao.
Bibi huyo alijifungua katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Lagos.
Akitoa tangazo hilo Jumapili, mwenyekiti wa baraza la ushauri la chuo hicho, Profesa Wasiu Adeyemo, alisema kuwa mwanamke huyo alijifungua kwa njia ya ''upasuaji baada ya wiki 37 za ujauzito''.
Mume wa mwanamke huyo Noah Adenuga ameiambia BBC kuwa iliwachukua miaka 43 kutafuta mtoto na kwamba waliwahi hata kutumia njia ya kuanguliwa kwa mayai yake ya uzazi nje ya mfuko wa uzazi na baadae kuchanganywa na mbegu za kiume na kisha kupandikizwa ndani ya mfuko wake wa uzazi ama IVF kwa lugha ya kitaalamu mara kadhaa bila mafanikio.
Hata safari hii pia mafaniko yao yamepitia njia hiyo ya IVF.
Mama na watoto wake wachanga wanaendelea vema na kwa sasa wameruhusiwa kuondoka hospitalini.
Bwana Adenuga anasema safari yao ya kutafuta watoto iliwapeleka hadi nchini Uingereza na kuwarejesha tena Nigeria na imani yao iliwafanya waendelea kushi pamoja kwa miaka mingi bila watoto.
Adenuga mwenye umri wa miaka 70 pia anasema kuwa alipokea jumbe kutoka kwa kikundi cha madaktari wa uzazi ambao walisema matendo yake ni kijinga.
Daktari aliyemuhudumia mama huyo Adeyemi Okunowo alitaja kuzaliwa kwa watoto hao ' muujiza' lakini pia alisema mume huyo na mke wake walijiweka hatarini kwa kuamua kusaka mtoto katika umri wao mkubwa.
Utawala wa hospitali ulisema kuwa usingewaatia huduma ua IVF katika umri wa miaka 68 lakini waliamua kumlaza tu kwa sababu ulikua ni wajibu wao wa kimatibabu.
Wakati huo huo, wazazi hao wapya wameruhusiwa kuondoka hospitalini na mama na watoto wake wanaendelea vyema.
Hii si mara ya kwanza kwa mwanamke kikongwe kujifungua duniani.
Mwanamke mwingine nchini India kwa jina Mangayamma Yaramati alijifungua mwaka jana Septemba watoto pacha pia akiwa 73 katika jimbo la Kusini la Andhra Pradesh.
