Mazungumzo kuhusu bwawa la Ethiopia kuanza tena

Ethiopia, Sudan na Egypt, zinatarajiwa kuanza tena mazungumzo kuhusu bwawa la kuzalisha umeme la Ethiopia, lililojengwa kwa gharama ya dola bilioni 4 kwenye mto Nile, linalokabiliwa na utata.

Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed, ameandika ujumbe wa twitter kwamba mawaziri wa maji wa nchi hizo tatu watakutana kutafuta makubaliano ambayo kila nchi itapata haki yake inayostahili bila yeyote kupoteza chochote. Hata hivyo tarehe rasmi ya mkutano huo haijatangazwa. Bwawa hilo lipo karibu na mpaka wa Ethiopia na Sudan.

Kwa upande wake Misri, inayotegemea kwa asilimia 90 maji ya mto Nile, ina wasiwasi kwamba kufunguliwa kwa bwawa hilo kutaathiri kiwango cha maji katika mto Nile.

Ethiopia ilijiondoa katika mazungumzo yaliokuwa yakisimamiwa na Marekani kuhusu bwawa hilo.

Ethiopia iliishutumu Marekani kwa kukiuka jukumu lake kama mpatanishi asiyeegemea upande wowote, kwa kusema kwamba ujenzi wa bwawa hilo haustahili kukamilika bila makubaliano. Ujenzi wa bwawa la Ethiopia ulianza mwaka 2011.