Sheria Yaokoa 30 Waliopata Ujauzito Kuendelea Na Masomo

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema Sheria ya Kuwalinda Wari na Mtoto wa Mzazi mmoja Namba 4 ya mwaka 2005, imewawezesha wanafunzi 30 waliopata ujauzito kuendelea na masomo yao Unguja na Pemba.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pemba Juma alisema hayo wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2020/2021.

Alisema sheria hiyo imeleta mabadiliko makubwa na ni mkombozi kwa watoto wa kike waliopata matatizo ya ujauzito, lakini imetoa nafasi ya kuwarudisha shule na kuendelea na masomo. Juma alisema wapo wanafunzi waliopata ujauzito na kufaidika na sheria hiyo, wamekubali kurudi shule na kuendelea na masomo, ambapo wapo waliofaulu hadi kidato cha sita na kuendelea vyuo vikuu.

Alisema kesi za ndoa 13 zimeripotiwa katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, ambapo kwa mujibu wa Sheria ya Elimu ya mwaka 1982 Kifungu 20 (3), wanafunzi hao walifukuzwa shule kwa sababu wapo katika elimu ya lazima.

“Spika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali itaendelea kutekeleza sheria ya wanafunzi wanaopata ujauzito kuendelea na shule ambayo tumeibaini kuleta mabadiliko makubwa ya maendeleo ya wanafunzi hao,” alisema.

Juma alisema Wizara ya Elimu imejipanga kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia, ikiwemo kuwadhalilisha wanafunzi wa kike. Aliwataka walimu kuhakikisha wanafuata maadili na kujiepusha na vitendo vya ukatili wa kijinsia, ikiwemo kuwapa mimba wanafunzi wa kike.

“Matukio ya walimu kuwapa mimba wanafunzi yamepungua sana kwa sababu walimu sasa wanajifahamu na kuyajua majukumu yao kama ni walezi wa wanafunzi wanapokuwa katika maeneo ya shule,” alisema.

Mapema alisema Wizara ya Elimu ipo katika mchakato wa kuandaa rasimu ya Sheria ya Elimu na tayari imepelekwa kwa wadau kwa ajili ya kujadiliwa.