Polisi mjini Paris, Ufaransa imefanya misako iliyoilenga mitandao ya Waislamu wa itikadi kali baada ya tukio la kuchinjwa kwa mwalimu mmoja wa somo la historia siku tatu zilizopita.
Mwalimu huyo alichinjwa baada ya kuwaonyesha wanafunzi wake kibonzo cha Mtume Muhammad. Mauaji yake yamezua hasira nchini Ufaransa na hapo Jumapili mamia kwa maelfu ya watu walishiriki maandamano kote nchini humo ya mkumbuka mwalimu Samuel Paty pamoja na kutetea uhuru wa kujieleza.
Kufuatia maandamano hayo, Waziri wa Mambo ya Ndani Gerald Darmanin ameahidi serikali ya Ufaransa haitapoteza muda kuwashughulikia wale aliowaita maadui wa taifa hilo.
Watu 15 wamewekwa kizuizini hadi sasa, ikiwa ni pamoja na wanafunzi wanne ambao wanaweza kuwa walimsaidia muuaji wa mwalimu huyo.
