Na Ezekiel Mtonyole - Dodoma.
Wazara ya Elimu Sayansi na Teknolojia kupitia taasisi ya elimu hapa nchini imeanza kupokea maoni ya wadau kuhusu maboresho ya mitaala inayotumika katika kufundishia hapa nchini ili mitaala hiyo iwe rafiki kwa wanafunzi kupata ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.
Akizindua kongamano lililolenga kupokea maoni ya wadau Naibu Wazari ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Omary Kipanga amesema serikali itaendelea kufanya kazi na wadau wa elimu kwa karibu ili kuzidi kuimarisha mfumo wa elimu ya Tanzania na kuhakikisha vijana wa Kitanzania wanapata maarifa, ujuzi na stadi za kazi stahiki.
Kipanga amewahakikishia wadau wa elimu kuwa Serikali itaendelea kufanya kazi nao kwa karibu ili kuzidi kuimarisha mfumo wa elimu ya Tanzania na kuhakikisha vijana wa Kitanzania wanapata maarifa, ujuzi na stadi za kazi stahiki.
Aidha,Kipanga ameihimiza Bodi ya Taasisi ya Elimu Tanzania kuhakikisha inafuatilia kwa karibu na kuyafanyia kazi kikamilifu maoni yanayotolewa na wadau wa elimu kuhusu uboreshaji wa mitaala hiyo ili lengo la uboreshwaji mitaala hiyo liweze kufanikiwa.
“Niwahimize Bodi ya Elimu Tanzania kuhakikisha inafuatilia kwa karibu maoni ya wadau na kuyafanyia kazi kikamilifu na kwa umakini mkubwa ili tuweze kufanikiwa katika uboreshaji mitaala hii,” amesisitiza Mhe. Kipanga.
Mhe. Kipanga amewataka wadau wa elimu kuendelea kutoa maoni na mapendekezo yao kupitia majukwaa yaliyopo ya kutolea maoni ili kuisaidia Serikali kuwa na mitaala bora na inayokidhi matarajio ya Watanzania.
Hata hivyo amewataka washiriki wote wa kongamano hilo kushiriki kikamilifu kutoa maoni yao ambayo yatafanyiwa uchambuzi wa kitaalamu kwa lengo la kupata mitaala bora itakayolenga kwenye ujenzi wa ujuzi kwa wahitimu.
“Ni imani yangu kupitia mkutano huu mtatoa maoni na mapendekezo yatakayowezesha Serikali kuwa na mitaala iliyo bora zaidi na itakayokidhi matarajio ya Watanzania kwa ujumla,” amesema Mhe. Kipanga.
Amesema uamuzi wa kuboresha mitaala hiyo umetokana na kukua kwa maendeleo na mabadiliko ya dunia huku akisisitiza kuwa serikali imezingatia pia malalamiko ya wadau.
“Mimi niwaombe tu muwe huru katika kutoa maoni kwa sababu yatasaidia katika kufanya elimu yetu kuboreka na kupata wahitimu tunawataka ambao watamaliza shule wakiwa na ujuzi wao tayari.
Kwa upande wake,Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo amewashukuru wadau waliofika kwenye mkutano huo na kuwataka wadau wote nchini ambao hawakuweza kuhudhuria mkutano huo, kuwasilisha maoni yao kupitia fomu zilizopo kwenye tovuti ya Taasisi ya Elimu Tanzania (www.tie.go.tz) na namba ya simu 0735041169.
“Kwa kuzingatia hili napenda kumshkuru Rais Samia kwa maelekezo ambayo ametoa kwa niaba ya Wizara kuhakikisha kazi hii inafanyika kwa weledi mkubwa,wadau wote mshiriki kikamilifu katika kutoa maoni,”amesema Dk Akwilapo.
Awali Mkurugenzi Mkuu wa TET, Dk. Aneth Komba amesema wanatarajia kuwa wadau watapata uelewa wa pamoja kuhusu maboresho ya mitaala hiyo ili watoe maoni yenye tija kwa elimu yetu nchini.
“Na imani kuwa tutapata maoni mengi yatakayoboresha Elimu yetu nchini,hivyo tushirikiane kuhakikisha tunafanikisha ubora wa elimu yetu kwa watoto ambao ni viongozi wajao wa taifa hili,” amesema Dk. Komba.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya TET, Profesa Bernadetha Killiani, amesema taasisi hiyo imejipanga kuhakikisha inaboresha mitaala kuendana na mahitaji ya sasa na kuzingatia maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Akitoa maoni yake katika mkutano huo, Diwani wa Kata ya Mtumba, Edward Maboje (CCM) amesema kuwa haoni kama kuna tatizo kwenye mitaala bali anaona tatizo lipo kwenye utekelezaji wake kwa kuwa kuna uhaba wa madawati, vitendeakazi na miundombinu hafifu
