Wanaharakati wa haki za wanawake Rwanda wasitisha tamasha la Koffi Olomide

 


Wanaharakati wa haki za wanawake nchini Rwanda wamesitisha tamasha la nyota wa muziki wa Congo Koffi Olomide kwa tuhuma za ubakaji na unyanyasaji wa kingono anazokabiliwa nazo katika mahakama za Ufaransa.


Mwezi Desemba, mahakama ya Paris itatoa uamuzi wa rufaa iliyoombwa kwa mashtaka dhidi ya nyota huyo, ambaye alikuwa amepatikana na hatia hapo awali, lakini amekuwa akikanusha madai ya wachezaji wake wanne wa zamani.


Juliette Karitanyi, mwanaharakati mjini Kigali, anasema kumruhusu Koffi kutumbuiza nchini Rwanda itakuwa "kutoheshimu waathiriwa wa unyanyasaji wa kingono".


BBC ilizungumza na waandaaji wa tamasha lakini hawakuzungumzia madai ya wanaharakati hao.


"Inaniuma zaidi kwamba tunamruhusu kutumbuiza hapa ilhali leo (Alhamisi) Rwanda imezindua siku 16 za harakati za kukomesha Unyanyasaji wa kijinsia" - Bi Karitanyi aliambia BBC.


Wengine kwenye mitandao ya kijamii hata hivyo wanasema kuwa hakuna msingi wa kisheria wa kumzuia nyota huyo wa Rumba kutumbuiza nchini Rwanda.


Vincent Karega, balozi wa Rwanda nchini DR Congo amesema kwenye Twitter kwamba "mapokezi makubwa yanamngoja" nyota huyo mwenye umri wa miaka 65 nchini Rwanda.


Wakati Emma Uwingabire, mkazi wa Kigali anaiambia BBC kwamba "ni kinyume cha maadili kwa nchi ambayo inasema inawainua wanawake" kumkaribisha Koffi Olomide.

Post a Comment

0 Comments