Wafanyakazi walia na Kikotoo na mishahara.




Na John Walter -Babati 
 Wafanyakazi wameiomba serikali kushughulikia changamoto waliyonayo kwa muda mrefu juu ya kikokotoo cha mafao pindi wanapostaafu.

Akizungumza katika maadhimisho ya Meimosi yaliyoandaliwa na shirikisho la vyama la Wafanyakazi (TUCTA) mkoa wa Manyara yaliyofanyika April 29,2024 uwanja wa Tanzanite Kwaraa mjini Babati , Katibu wa TUICO mkoa wa Manyara Juma Makanyaga  amesema hawaridhishwi na kikotoo kilichopo cha asilimia 33.3 kwani kimekuwa ni mateso kwa watumishi na kupelekea sintofahamu kubwa kwa wafanyakazi na mustakabali wa maisha yao.

Wamemuomba Rais Samia Suluhu Hassan alitazame jambo hilo kwa jicho la tatu kwani kinachotumika hakiakisi hali halisi ya wanachama na kupendekeza kifanyiwe mabadiliko au  kirudishwe kikotoo cha asilimia 50 ili kukidhi matakwa yao.


Katika hatua nyingine wameiomba serikali ifike Mahali ione umuhimu wa kuboresha mishahara kwa wafanyakazi wote.

Aidha wameiomba ofisi ya Katibu tawala mkoa wa Manyara kuishirikisha ofisi ya Shirikisho la Wafanyakazi katika shirikishwa  masuala mbalimbali kwani ni muda mrefu serikali imeshindwa kufanya hivyo.

Kwa upande wake mgeni Rasmi mkuu wa wilaya ya Babati Lazaro Twange amesema amepokea maelekezo kutoka kwa katibu tawala mkoa kwamba Mei 3,2024 atakutana na Wafanyakazi wote kwa ajili ya kuwasikiliza na kutatua changamoto zilizopo.



Kuhusu mishahara kupanda na kikotoo amewataka Wafanyakazi waendelee kuwa watulivu wakati huu serikali inapotafuta ufumbuzi na kwamba Mei mosi jijini Arusha atakapokuwa akihutubia Rais Samia Suluhu Hassan huenda akazungumza jambo.

Sherehe za Mei mosi mwaka huu kitaifa zinafanyika mkoani Arusha na mgeni Rasmi atakuwa Samia Suluhu Hassan Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kauli mbiu ya Mei mosi 2024 “Nyongeza ya Mishahara ni Msingi wa Mafao Bora na Kinga Dhidi ya Hali Ngumu ya Maisha”

Post a Comment

0 Comments