F BAWASA na RUWASA Wajipanga Kutekeleza Ilani ya CCM 2025–2030 | Muungwana BLOG

BAWASA na RUWASA Wajipanga Kutekeleza Ilani ya CCM 2025–2030


Na John Walter-Manyara

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Babati (BAWASA) na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoa wa Manyara zimekubaliana kushirikiana kwa karibu katika utekelezaji wa miradi ya maji kwa lengo la kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kazi cha sekta ya maji kilichofanyika mjini Babati, kikibeba kauli mbiu isemayo “Pamoja tujenge huduma bora za maji kwa maendeleo ya mkoa wa Manyara.”

Kikao hicho kimewakutanisha wakuu wa taasisi hizo wakiongozwa na Meneja wa RUWASA Mkoa wa Manyara, Mhandisi James Kionaumela, pamoja na Mkurugenzi wa BAWASA, Mhandisi Iddy Msuya, ambapo wamejadili mikakati ya kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika maeneo ya mijini na vijijini mkoani humo.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhandisi Kionaumela amesema ushirikiano kati ya RUWASA na BAWASA utaongeza ufanisi, kupunguza changamoto za utekelezaji wa miradi na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ya maji kwa wakati.

Kwa upande wake, Mhandisi Msuya amesema kuwa hadi sasa huduma ya maji katika mji wa Babati imefikia asilimia 85, huku kiwango cha upatikanaji wa maji kwa mkoa mzima wa Manyara kikiwa ni asilimia 75, hali inayotoa msingi mzuri wa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mipya na ya maboresho.

Mkuu wa Maabara ya maji mkoa wa Manyara Nicolaus Germanus, amesema hali ya ubora wa maji katika mkoa wa Manyara inaridhisha.

Naye Mhandisi wa maji kutoka Bonde la maji, bonde la  kati katika ofisi ya Babati  Denis Gunze, amesema wameweka mikakati ya kuhakisha wanafanya utafiti juu ya upatikanaji wa maji sehemu yenye maji.


Viongozi hao wamesisitiza kuwa ushirikiano huo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM, sambamba na adhma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama kwa uhakika na hivyo kuwapatia tabasamu wananchi.

Kwa mujibu wa Ilani ya CCM 2025–2030, mkoa wa Manyara unatarajiwa kufikia kiwango cha upatikanaji wa huduma ya maji kwa asilimia 99 ifikapo mwaka 2030, lengo ambalo BAWASA na RUWASA wameahidi kulifanyia kazi kwa nguvu, ubunifu na mshikamano.

 


Chapisha Maoni

0 Maoni