F Manyara wazindua namba ya bure ya huduma kwa mteja. | Muungwana BLOG

Manyara wazindua namba ya bure ya huduma kwa mteja.

 


Na John Walter-Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amezindua rasmi namba ya bure ya huduma kwa mteja itakayokuwa ikitumika kupokea changamoto, kero na malalamiko ya wananchi wa mkoa wa Manyara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Sendiga amesema namba hiyo ambayo ni 0800 787 722 imelenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kutoka kwa wananchi kwa wakati, ili changamoto zinazowakabili ziweze kushughulikiwa kwa haraka na ufanisi. Ameeleza kuwa mwananchi atakuwa na uhuru wa kupiga namba hiyo bila malipo au makato yoyote na kutoa taarifa sahihi bila kudanganya.

“Mfumo huu utaimarisha uwajibikaji na uwazi katika utoaji wa huduma kwa wananchi, kwani utasaidia serikali kupata taarifa za moja kwa moja kutoka kwa wananchi na kuzifanyia kazi kwa wakati,” amesema Sendiga.

Aidha, Mkuu wa Mkoa amezitaka ofisi zote zilizo chini ya uongozi wake kuhakikisha zinashughulikia kwa haraka changamoto zote zitakazopokelewa kupitia namba hiyo. Ameelekeza kuwa baada ya kuzifanyia kazi, taarifa hizo zirudishwe katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa ajili ya kuhifadhi kumbukumbu, maandalizi ya ripoti na ufuatiliaji wa taarifa za kila mwezi.

Uzinduzi wa namba hiyo ya bure unatarajiwa kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za serikali na kuimarisha ushirikiano kati ya wananchi na viongozi katika Mkoa wa Manyara.

 


Chapisha Maoni

0 Maoni