F Mtoto wa Miaka Minne Afariki Dunia kwa Kugongwa na Gari Hanang. | Muungwana BLOG

Mtoto wa Miaka Minne Afariki Dunia kwa Kugongwa na Gari Hanang.


Na John Walter-Hanang'

Mtoto wa miaka minne, Abdilahi Hussein, amefariki dunia leo baada ya kugongwa na gari katika Kijiji cha Endagaw, Kata ya Endagaw, Wilaya ya Hanang mkoani Manyara.

Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa, tukio hilo limetokea wakati mtoto huyo akitoka nyumbani kwao kuelekea dukani kwao, ambalo lipo upande wa pili wa barabara kuu inayoelekea Singida.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Endagaw, Rajabu Mande, amesema kuwa kifo cha mtoto huyo ni pigo kubwa kwa jamii, akieleza kuwa mtoto huyo alikuwa nguvu kazi ya taifa la kesho, lakini maisha yake yamekatizwa kutokana na dereva kushindwa kuchukua tahadhari katika eneo la makazi ya watu.

Taarifa zinaeleza kuwa mtoto huyo aligongwa akiwa pembeni ya barabara, na baadaye alikanyagwa maeneo ya kichwani, hali iliyosababisha kifo chake papo hapo.

Mashuhuda wa tukio hilo wameeleza masikitiko yao na kuomba mamlaka husika kuchukua hatua kali dhidi ya madereva wasiotii sheria za usalama barabarani, hasa katika maeneo yenye makazi ya watu, ili kuzuia ajali zinazogharimu maisha ya wananchi wasio na hatia.

Jamii ya Endagaw imeendelea kuomboleza msiba huo, huku wito ukitolewa kwa madereva wote kuongeza umakini na kuzingatia sheria za barabarani ili kulinda maisha ya watoto na watumiaji wengine wa barabara.

 

Chapisha Maoni

0 Maoni