F TARURA Manyara yaendelea kutekeleza miradi ya madaraja kwa ufadhili wa World Bank | Muungwana BLOG

TARURA Manyara yaendelea kutekeleza miradi ya madaraja kwa ufadhili wa World Bank


Na John Walter-Manyara

Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imeendelea kutekeleza miradi ya ujenzi wa madaraja katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo kwa lengo la kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi kwa wananchi, hususan kipindi cha mvua.

Akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Mbulu, Mhandisi Nuru Hondo amesema jumla ya shilingi bilioni 1.4 zimetolewa na Benki ya Dunia (World Bank) kwa ajili ya ujenzi wa madaraja matatu ambayo ni daraja la Isale, Marish pamoja na Haydom 102 ndani ya Wilaya ya Mbulu.

Amesema miradi hiyo inalenga kuondoa changamoto ya mawasiliano na usafirishaji ambayo imekuwa ikiathiri wananchi kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Dudiyek Kata ya Imboru, Paskali Thomas amesema wananchi wanasubiri kwa hamu kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa daraja katika maeneo hayo akibainisha kuwa kipindi cha mvua wamekuwa wakipata mateso makubwa kutokana na kukosa huduma muhimu kama afya, elimu na masoko kwa sababu ya kukatika kwa mawasiliano.

“Msimu wa mvua tunateseka sana, hatuwezi kuvuka, wagonjwa wanashindwa kufika hospitali, wanafunzi wanashindwa kwenda shule na hata shughuli za kiuchumi zinasimama.

Tunashukuru TARURA kwa kutusikiliza na tunasubiri kwa matumaini makubwa mradi huu,” amesema Paskali Thomas.

Aidha, ameipongeza TARURA kwa usimamizi mzuri wa miradi hiyo na kuhakikisha inatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa. 

Ameongeza kuwa miradi hiyo imechangia kutoa ajira kwa vijana wa eneo hilo, ambapo zaidi ya shilingi milioni 400 zimetumika katika mradi wa World Bank, hatua inayosaidia kuinua kipato cha wananchi na kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira.

Wakati huo huo, Meneja wa TARURA Mkoa wa Manyara, Mhandisi Salim Bwaya, alifanya ziara ya kukagua miradi hiyo akiambatana na menejimenti nzima ya TARURA mkoa, kwa lengo la kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji. 

Katika ziara hiyo, aliwasisitiza wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha ujenzi wa madaraja kwa wakati uliopangwa na kwa ubora unaotakiwa ili wananchi waweze kunufaika na miradi hiyo kwa haraka.

Mhandisi Bwaya amesema ujenzi wa madaraja hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo, hususan World Bank, katika kuboresha miundombinu ya barabara na madaraja ili kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo ya vijijini.

Miradi ya madaraja inayoendelea katika Wilaya ya Mbulu inatarajiwa kuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi, kwa kuboresha usafiri, kuongeza upatikanaji wa huduma za jamii na kuimarisha shughuli za kibiashara katika ukanda huo wa Mkoa wa Manyara.


PICHA MBALIMBALIU WAKATI WA ZIARA HIYO.














 

Chapisha Maoni

0 Maoni