Na John Walter-Babati
Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya Wilaya ya Wilaya ya Babati, Januari Bikuba, ametoa wito kwa jamii kukemea kwa nguvu vitendo vya ukatili wa kijinsia na kuhakikisha wahusika wanachukuliwa hatua za kisheria bila upendeleo.
Akizungumza Februari 12, 2026 katika mkutano wa hadhara
uliofanyika Kijiji cha Magugu, Bikuba amesema ukatili wa kijinsia haufai
kufumbiwa macho hata kidogo na kuwataka wananchi kuendelea kutoa taarifa za
matukio hayo bila kusahau kutumia namba ya msaada 116.
Katika mkutano huo, baadhi ya wanaume wameeleza kuwepo kwa
changamoto kwa waathirika wa ukatili, hususan wanaume, wakidai kuwa wanapofika
vituo vya polisi kutoa taarifa mara nyingine hawasikilizwi na wakati mwingine
kufukuzwa.
Bikuba ameisisitiza kuwa matukio ya ukatili wa kijinsia ni
uhalifu kama ilivyo kwa makosa mengine ya jinai, hivyo jamii inapaswa kutoa
taarifa mapema na kuwa tayari kutoa ushahidi mahakamani ili sheria iweze
kuchukua mkondo wake dhidi ya wahusika.
Ameongeza kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia
yanahitaji ushirikiano wa wadau wote, wakiwemo viongozi wa jamii, familia na
vyombo vya dola, ili kuhakikisha kila mwathirika anapata haki bila kujali
jinsia yake.
Aidha, amewahimiza wananchi kuachana na tabia ya kuficha
matukio ya ukatili majumbani, akieleza kuwa kufanya hivyo kunachangia kuendelea
kwa vitendo hivyo na kudhoofisha juhudi za serikali za kulinda haki za
binadamu.
Naye mkuu wa Kituo cha Polisi Magugu amesema baadhi ya
waathirika wa ukatili hushindwa kufuatilia kesi hadi mahakamani kutokana na
kupewa hongo, hali inayokwamisha mwenendo wa mashauri na wakati mwingine
kusababisha kesi kuondolewa kabisa mahakamani.
0 Maoni