Magonjwa ya fangasi sehemu za wazi

Kama mwendelezo wa makala yetu ya maradhi ya ngozi, tuendelee kuangalia maradhi ya ngozi yanayosababishwa na fangasi hasa wale  wanaoshambulia sehemu za wazi za mwili, yaani Tinea corporis.

Fangasi wa ngozi ya mwili
Aina hii ya fangasi huathiri sehemu zisizojificha (sehemu za nje za mwili), tofauti na aina ya fangasi tuliozungumza wiki zilizopita ikiwemo wiki iliyopita tulipotazama fangasi wanaokaa sehemu za siri za mwili na zile zilizojificha kama vile, katikati ya vidole au chini ya kucha.

Aina hii ya fangasi huathiri sehemu za mwili ambazo ziko wazi kwa mfano tumboni au mgongoni.

Fangasi hawa hushambulia sehemu gani?
Fangasi wa aina hii huwa na uwezo wa kushambulia sehemu kubwa zaidi ya mwili kama mikono, miguu, uso na kiwiliwili.

Mwonekano wake
Fangasi wa aina hii huonekana kwenye mwili wakiwa na muundo wa duara mfano wa sarafu (mitaani tumezoea kusema shilingi) na ngozi ikiwa imevimba kwenye uzio wa eneo ambalo fangasi amevamia, yaani ukiangalia eneo lenye athari utaona kuna ka duara, mfano wa sarafu ambako kamevimba kwenye kingo za duara hilo mfano wa pete.

Eneo lenye maradhi pia hubadilika rangi na kuwa na rangi tofauti kidogo na rangi ya ngozi ya eneo ambalo halijaathirika na maambukizi. Mfano, mtu ambaye ana ngozi ya maji ya kunde eneo ambalo limeathirika linaweza kuwa na rangi nyeusi zaidi au likawa na rangi nyaupe zaidi.

Dalili za maambukizi
Aina hii ya fangasi huwa na dalili chache sana na kubwa ni muonekano wake kama nilivyouelezea hapo juu. Ila vifuatavyo huonekana :-

  • Kubadilika kwa rangi ya ngozi ya eneo lenye maambukizi
  • Eneo la ngozi lenye maambukizi huwa lina muundo wa duara mfano wa sarafu ya fedha.
  • Ngozi kubanduka kwenye eneo lenye maambukizi
  • Ngozi kukauka kwenye eneo lenye maambukizi
  • Inawezekana kabisa kupata muwasho kwenye eneo lililo na maradhi ingawa si sehemu zote za mwili zenye maambukizi zinaonyesha dalili hii.

Husambaa vipi
Kati ya aina zote za fangasi aina hii ni rahisi zaidi kuambukizwa kutoka kwa mtu mwenye maradhi kwenda kwa Yule asiye na maradhi.

Maradhi haya huambukizwa kwa njia zifuatazo:

  • Kugusana na mtu mwenye maambukizi ya fangasi hawa
  • Kugusa vitu vilivyobeba fangasi wa aina hii kama vile nguo ikiwemo nguo za ndani, chanuo la nywele, mikufu, vifaa vya kuogea, viatu, soksi
  • Unaweza kupata maambukizi pia kwa kugusa sehemu ambazo mwenye maradhi amegusa kama ukuta, viti, makochi na vitu vingine.
  • Wanyama wa kufugwa pia wanaweza kubeba vimelea hivi vya fangasi.

Nani yuko hatarini
Watu ambao huweza kupata maambukizi ya fangasi wa aina hii ni kama wafuatao:

  • Wale wanaofanya kazi zinazohusisha kugusana na watu wenye maambukizi ya fangasi
  • Wanaolala kitanda kimoja na wenye maambukizi ya fangasi wa aina hii
  • Wanaoshiriki mapenzi na wenza wenye maambukizi ya fangasi hao