https://monetag.com/?ref_id=TTIb 7 mbaroni kwa tuhuma za kuiba mil 405/- za saccos | Muungwana BLOG

7 mbaroni kwa tuhuma za kuiba mil 405/- za saccos

WATUMISHI saba wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga ambao ni wajumbe wa Bodi ya Chama cha Ushirika Mbinga Kurugenzi Saccos wamekamatwa na Jeshi la Polisi wakituhumiwa kuiba Sh 405,204,514 za wanachama wa chama hicho na kusababisha kishindwe kujiendesha.

Aidha, hatua hiyo ya kukamatwa kwa wajumbe hao ilitolewa na Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoani humo, Biezery Malila baada ya kusomwa taarifa ya ukaguzi ya chama hicho iliyobainisha wizi wa fedha hizo katika Mkutano Mkuu Maalumu wa Wanachama uliofanyika Januari 21, mwaka huu mjini hapa.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Zubery Mwombeji aliwataja watumishi hao saba waliowekwa mahabusu mpaka sasa kuwa ni Zackaria Lingowe, Emmanuel Mwasaga na Alex Kalilo ambao ni watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, Jamima Challe na Stella Mhagama wanatoka Halmashauri ya Mji wa Mbinga, Lucas Nchimbi na Mhadisa Meshack pia wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga, ambao bado wanashikiliwa na Jeshi la Polisi wakiendelea kuhojiwa kutokana na tuhuma zinazowakabili.

“Kwa masikitiko makubwa ndugu zangu naomba niwaeleze kwamba mwenendo wa chama hiki sio mzuri kwa kuwa wajumbe wa bodi hii wameshiriki kwa namna moja au nyingine kukiuka taratibu,” alisema Mrajisi Malila.

Mrajisi huyo alifafanua kuwa fedha hizo ambazo wajumbe hao wanadaiwa kujinufaisha kwa matakwa yao binafsi, zilitokana na mkopo wa Sh milioni 500 uliotolewa na Benki ya CRDB kwa ajili ya kukopeshwa wanachama, lakini cha kushangaza waliamua kuzitumia kinyume cha taratibu husika.

Alimtaja mtuhumiwa mwingine ambaye sio mtumishi wa serikali kuwa ni Meneja wa Saccos hiyo Raymond Mhagama ambaye ametoroka huku akikabiliwa na kesi ya ubadhirifu aliyofunguliwa jadala Kituo kikuu cha Polisi Mbinga.