TCRA yahadharisha utumaji fedha holela mtandaoni

MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa tahadhari kwa watumiaji wa huduma za mawasiliano juu ya utapeli unaofanywa kwa kutumia simu za mkononi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kaimu Meneja wa Mawasiliano kwa Umma wa TCRA, Semu Mwakyanjala alisema kumekuwa na ongezeko la matapeli wanaoghushi utaratibu wa mawasiliano na kuwalaghai watu kutuma pesa kwa simu za mkononi.

Mwakyanyala alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya huduma za kifedha na kwa miezi miwili iliyopita ya Novemba na Desemba, 2016 kwa wastani kiasi cha jumla ya fedha iliyopita katika mitandao ya kampuni zinazotoa huduma za kifedha kwa njia ya simu za mikononi ni Sh trilioni 13.07.

Aliongeza kuwa ni vyema wananchi wakazingatia mambo mbalimbali kabla ya kutuma fedha, ikiwemo kutokutekeleza maagizo yoyote yanayohusu fedha kwa mawasiliano ya simu hata kama yanatoka kwenye namba ya mtu anayemfahamu badala yake ampigie aliyemtumia ujumbe kwa namba nyingine kufanya uhakiki.

Pia aliwataka wananchi pale wanapopokea taarifa kwa njia ya simu au ujumbe mfupi wa maandishi kuwa ametumiwa fedha kwa makosa na kufuatiwa na kutumiwa ujumbe mfupi unaofanana na ujumbe unaotumwa na watoa huduma na kutakiwa kurudisha fedha hizo, asifanye haraka badala yake wachukue tahadhari zote kujiridhisha na uhalali wa taarifa hiyo.

“Omba taarifa fupi ya akaunti yako kwa mtoa huduma uhakiki miamala yako na salio lako ikibidi wasiliana na kituo cha huduma kwa wateja cha mtoa huduma wako kwa kuwa kumekuwepo na uhalifu wa kulaghai watoa huduma za mawasiliano kwa kutumia ujumbe mfupi unaokaribia kufanana na ujumbe unaotumwa na watoa huduma,” alieleza.