Moses Misiwa
Baada ya kusomewa mashtaka hayo ambayo waliyakana, viongozi hao na wenzao Mwinyi Marwa (31) na Marwa Isamore (67), walinyimwa dhamana baada ya Jamhuri kuweka pingamizi na hivyo walipelekwa rumande.
Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Tarime, Martha Mpaze, Mwendesha Mashtaka Samwel Meriala alidai washtakiwa walitenda kosa la kufanya mkutano usio halali kinyume na sheria Februari 2.
Meriala alidai washtakiwa walitenda kosa hilo katika Kijiji cha Bisarwi kilichopo Kata ya Manga, ambako walifanya mkutano wenye nia ya kuzuia maendeleo ya kijiji yaliyopangwa, hivyo kuwafanya majirani na wananchi kupata hofu juu ya mkutano huo na kusababisha kuvunjika kwa amani.
Baada ya washtakiwa kukana mashtaka dhidi yao, Wakili wao, Evans Otieno aliiomba Mahakama iwapatie dhamana wateja wake kwa kuwa kosa linalowakabili kisheria na kikatiba linatoa haki ya kudhaminiwa.
Hata hivyo, Wakili wa Jamhuri, Valence Mayenga aliwasilisha pingamizi dhidi ya dhamana ya washtakiwa, akidai wakiachiwa watavuruga amani.
Wakili Otieno alipinga ombi hilo akidai halijapokewa mahakamani na halikuwa limepigwa muhuri wa Mahakama.
Baada ya mabishano ya kisheria, Hakimu Mpaze aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 7, atakapotoa uamuzi kuhusu maombi ya dhamana. Washtakiwa walipelekwa rumande.
