BAADA ya juzi kupata ushindi wa mabao 3-0, kikosi cha Timu ya Taifa ya Vijana umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) leo kinarudiania na yosso wenzao wa Burundi mchezo utakaofanyika kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Shime alisema kuwa amekubali timu yake icheze mechi ya pili ndani ya siku tatu kwa ajili ya kuwaandaa wachezaji wake na hali kama hiyo endapo itatokea watakapokuwa Gabon kwenye Fainali za Vijana za Afrika.
"Ni lazima wachezaji wawe tayari kupambana katika mazingira yote, hatujui ratiba itakavyokuwa, hatutaki kukariri, nashukuru tulipata ushindi jana (juzi) na kesho (leo) tunatarajia kupata matokeo mazuri," alisema Shime.
Baada ya mechi ya leo, yosso hao watarejea jijini Dar es Salaam kuendelea na mazoezi kwa ajili ya kuwasubiri Ghana ambao watacheza nao mechi ya kirafiki kwenye Uwanja wa Taifa.
Fainali za Vijana za Afrika zinatarajiwa kufanyika kuanzia Mei 14 na kabla ya hapo, Serengeti Boys itakwenda Morocco kuweka kambi ya mwezi mmoja.