Spika wa bunge Job Ndugai ameitaka Takukuru kujiandaa kukaguliwa hesabu zake na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali CAG kwani tangu kuanzishwa kwake haijawahi kukaguliwa licha ya kuidhinishiwa fedha nyingi za bajeti na Bunge.
Spika Ndugai amesema hayo wakati akizindua filamu ya bahasha iliyolenga kupinga vitendo vya rushwa na madhara yake iliyoandaliwa na Takukuru kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ambapo ameitaka taasisi hiyo nyeti ambayo pamoja na mambo mengine inahusika na wahujumu wa fedha za umma kukaguliwa kwani inatumia fedha za umma katika utekelezaji wa shughuli zake.
Katika uzinduzi huo Mwenyekiti wa kamati ya bunge ya maadili George Mkuchika amesema vita ya rushwa ni kubwa na inahitaji ushirikishwaji ili kuishinda kwa manufaa na maendeleo ya taifa.
Awali Naibu Mkurugenzi wa Takukuru Brigedia Jenerali John Mbungo amesema filamu hiyo itawafikia wananchi wengi kupitia njia mbalimbali ili kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu rushwa na madhara yake.
