Kesi ya akina Hanspope, Kaburu yapigwa kalenda tena


Mahakama  ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuondolea mashtaka mfanyabiashara Peter Lauwo aliyetakiwa kuunganishwa katika kesi ya utakatishaji fedha  pamoja na viongozi wa Simba na mfanyabiashara Hans Pope kwa sababu hayupo.

Hatua hiyo imekuja baada ya upande wa mashtaka kuwasilisha ombi la kumuondoa mshtakiwa Lauo chini ya kifungu cha 91 (1) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai.

Aliyewasilisha ombi hilo, Wakili wa serikali Mwandamizi, Shadrack Kimaro ameieleza mahakama kuwa, Lauo aliahidi kuwa angejisalimisha Takukuru Jana ili leo aletewe hapa mahakamani lakini hajatokea.

Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba amekubaliana na ombi na mashtaka dhidi ya Lauo yameondolewa nchini ya kifungu cha 91 (1) cha sheria mwenendo wa sheria ya makosa ya jinai.

Baada ya kuondolewa na Laou, upande wa mashtaka umewasomea maelezo ya awali (PH)  Rais wa klabu ya Simba, Evans Aveva, Makamu wake, Godfrey Nyange maarufu kama Kaburu na mfanyabiashara Hans Pope.

Akisoma PH, Kimaro amedai, Machi 12.2016 klabu ya Simba ililipwa USD 319,212 na Timu ya Etoile ya Tunisia kama Malipo ya mchezaji Emmanuel Okwi ambazo ziliwekwa kwenye benki ya CRDB tawi la Azikiwe account ambayo mtia saini wake alikuwa ni Aveva na Kaburu.

Amedai kuwa, Machi 3.2016 kiasi cha USD 300,000 zilihamishwa kwenda kwenye akaunti binafsi ya mshtakiwa Aveva iliyoko katika benki ya Barclays iliyopo mtaa wa Ohio ambayo Aveva ndio mtia saini baada ya kusainiwa na yeye Aveva pamoja na Kaburu.

Kimaro ameendelea kudai kuwa, uhamishwaji wa fedha hizo haukuwa na Baraka na ya kamati tendaji ya klabu ya Simba sababu fedha hizo zinadaiwa kuwa zilikopwa na klabu ya Simba.

Imedaiwa, fedha hizo zilianza kuamishwa kidogo kidogo, mwanzo Aveva alihamisha USD 62,183 kwenda kwa kampuni ya Ninah... Kama malipo ya kununua nyasi bandia kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa klabu ya Simba uliopo Bunju Kinondoni. Na kwamba USD zililipwa kwa Lauo kwa ajili ya kujenga uwanja huo huku wakijua kuwa kampuni ya Lauo haijasajiliwa na bodi ya wakandarasi.

Hata hivyo, washtakiwa Aveva na Kaburu walikubali anuani zao tu na kukana tuhuma zinazowakabili huku Hanspope akikubali anuani yake na kusema kuwa, ni kweli alifanya mchakato wa manunuzi ya nyasi bandia.

Katika kesi hiyo, washtakiwa wote wanashtakiwa na makosa kumi yakiwemo ya Kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo kula njama, matumizi mabaya ya madaraka, utakatishaji na kuwa kuwasilisha nyaraka za kughushi na kuendesha biashara bila sheria.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Oktoba 31, mwaka huu, kesi hiyo itakapoanza kusikilizwa.
Mpya zaidi Nzee zaidi

Popular Items