Okwi awatambia Yanga SC


Mshambuliaji wa Simba SC, Emmanuel Okwi amewatambia wapinzani wao Yanga SC kwa kuwaambia kwenye mechi tano zilizobakia watapambana kuchukua pointi zote 15 ili wachukue ubingwa kwa mara nyingine.

Okwi ambaye ameunda utatu hatari ndani ya klabu hiyo akishirikiana na John Bocco na Meddie Kagere ameliambia Championi Jumatano, kuwa malengo yao ni kupambana kwa nguvu kuhakikisha ubingwa walioutwaa msimu uliopita wanauchukua tena kwa msimu huu kwani ndiyo kombe pekee ambalo kwa sasa wanaligombania.

“Lengo letu ni kuiona timu inapambana kufikia kile ambacho kila mmoja anakitaka la kuchukua ubingwa kwa msimu huu, kwa sababu hilo ndilo kombe pekee ambalo lipo mbele yetu kwa sasa.

“Tunapambana kila mechi yetu kuhakikisha tunakusanya pointi tatu, na mechi hizi zilizobakia tutajituma zaidi ili tupate matokeo mazuri,” alisema Okwi.

Kwa sasa Simba wamebakisha michezo mitano ya ligi kuu huku wakiwa wanahitaji pointi nane pekee kwa ajili ya kutwaa ubingwa wa ligi, hadi jana walikuwa kileleni mwa msimamo wakiwa na pointi 82 ikiwa tofauti ya pointi mbili mbele ya Yanga ambao walikuwa nafasi ya pili na pointi 80.