Majeruhi 13 ajali ya moto waliolazwa Muhimbili hawajitambui


Majeruhi 13 kati ya 38 walionusurika katika ajali ya moto mkoani Morogoro waliolazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), hali zao zinadaiwa kuwa mbaya na wamelazwa katika Chumba cha wagonjwa Mahututi (ICU) wakiwa hawajitambui.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma hospitalini hapo, Aminieli Aligaesha, wagonjwa hao wako ICU wakiwa hawajitambui huku 25 wakiwa wanaendelea vizuri na waliofariki hadi sasa ni wanane.

“Hadi leo Agosti 13, hiyo ndiyo idadi ya wagonjwa waliolazwa MNH, na wale ambao wamefariki tayari miili yao imepelekwa Morogoro na mmoja umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti hapa Muhimbili,” amesema Aligaesha.

Wagonjwa waliofikishwa hospitalini hapo baada ya ajali walikuwa 39 wanaume wakiwa 35 na wanawake wanne.

Ajali hiyo ilitokea Jumamosi asubuhi eneo la Msamvu mkoani Morogoro baada ya lori la mafuta kuanguka na kulipuka na kusababisha vifo vya watu 75 na majeruhi zaidi ya 60.