Miradi yenye thamani ya Shilingi Trilioni 2.6 yazinduliwa na Mwenge


Jumla ya miradi 5,603 yenye thamani ya shilingi trilioni 2.6 imezinduliwa na Mwenge wa Uhuru kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka 2018.

Hayo yameelezwa Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Stella Ikupa alipokuwa akijibu swali la Mhe. Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum kuhusu idadi ya miradi inayofunguliwa na  Mwenge wa Uhuru kwa mwaka.

“Uwiano wa miradi inayozinduliwa kwa mwaka na kuwekwa mawe ya mzingi ni 1,402 yenye thamani ya shilingi 651,849,585,126.64,” amesema Ikupa.

Ameendelea kusema kuwa, miradi hiyo huendana na Kauli Mbiu mbalimbali. Mfano mwka 2017, Kauli Mbiu ilikuwa uwekezaji katika sekta ya viwanda. Mwaka 2018 Kauli Mbiu ilikuwa Uwekezaji katika Sekta ya Elimu, na  mwaka 2019 Kauli Mbiu ni Maji ni Haki ya Kila Mtu, Tutunze Vyanzo Vyake na Tukumbuke Kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Aidha, Waziri Ikupa amempongeza Mhe. Kadika kwa kukiri kuwa Mwenge wa uhuru umekuwa ukileta maendeleo makubwa nchini.