Rais wa Afrika Kusini hatashiriki mkutano wa UN

Raisi wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa hatahudhuria mkutano mkuu wa umoja wa mataifa jijini New York, baadae mwezi huu.

Badala yake, amesema atabaki nchini humo kushughulikia changamoto zinazokabili nchi yake kwa sasa ikiwemo vitendo vya mashambulizi ya chuki dhidi ya raia wa kigeni na unyanyasaji dhidi ya wanawake

Nchini Afrika Kusini, miongoni mwa vichwa vya habari juma lililopita ilikuwa ni taarifa kuhusu ubakaji na mauaji ya wanawake na watoto katika sehemu kadhaa za nchi.

Iliwaacha wanawake wengi wakijiuliza: "Je! nitafuata mimi!

Kesi moja iliyemhusisha mtu mwenye hadhi kubwa, mfanyakazi wa ofisi ya posta ambaye alikiri kubaka na kumuua mwanafunzi wa miaka 19 Uyinene Mrwetyana. Ilikuwa ni wakati ambao uliwafanya wanawake kuhisi hatari na hofu.

Takwimu za hivi karibuni za uhalifu, ambazo zilitolewa Alhamisi, zilidhihirisha kwamba hofu yao ni dhahiri. Mauaji, ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia vimeongezeka.


Lakini wanawake wengi wanakataa kunyamazishwa. Siku ya Ijumaa, mamia ya wanawake, ambao walikuwa wamevaa mavazi ya rangi nyeusi, walianza kukusanyika Johannesburg saa za asubuhi ili kuongeza uelewa dhidi ya dhuluma ya kijinsia.

Wanawake wengi walikuwa wakilia. Baadhi ya waandamanaji walikua wamebeba mabango yakiwa na ujumbe wa kuomba kukomeshwa kwa vitendo hivyo.