RC Ayoub aagiza Jeshi la Polisi kumkamata msanii wa Bongo Fleva Baby J



Na Thabit Madai,Zanzibar.

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharib Unguja, Ayoub Mahamed  Mahmoud ameliagiza Jeshi la Polisi ndani ya Mkoa huo kumkamata Msaani wa Bongo fleva Jamillah Abdallah alimarufu Baby J na Mwenzake Maulid Husein Abdallah (Mauzinde) kwa tuhuma za Uvunjifu wa maadili.

Ayoub aliagiza Jeshi hilo kuwakamata wahusika hao ndani ya siku tatu kwa ajili ya kuhojiwa zaidi na kchukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria za Nchi.

Agizo hilo la Mkuu huyo wa Mkoa limekuja kufuatia video zinazosambaa mitandao zikionesha vitendo vya uvunjifu wa maadili zilizofanywa mnamo tarehe 08 Septemba mwaka huu huko kiembe samaki katika sherehe ya singo iliyoandaliwa na Msaani huyo.

Akizungumza  na waandishi wa habari leo ofisini kwake Vuga, Mkuu wa mkoa  alisema kuwa vitendo hivyo vilivyofanyika katika sherehe hiyo  ni kinyume na Sheria, utaratibu wa Nchi.

Alisema vitendo kama hivyo haviwezi kuvumilika kutokana ni  ni kinyume na sheria taratibu, mila na utamaduni wa kizanzibar na hata Tanzania kwa ujumla.

"Natoa siku tatu tu kwa Jeshi la polisi kuwakamata na kuwaweka ndani wahusika waliopelekea kutokea kwa vitendo hivi vya uvunjifu wa maadili vinavyopelekea kutia dosari Zanzibar" alisema Rc Ayoub.

Aliongeza kusema kuwa agizo hilo amelitoa kutokana kuwa vitendo vilivyofanywa  katika sherehe hiyo ya singo havivumiliki hata kidogo, vinaharibu mila na silka za kizanzibar.

Aidha Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa yeye ni mlezi wa vijana na yupo karibu na vijana wengi lakini kwa kitendo kilichofanywa na msaani huyo katika sherehe aliyoiandaa hakivumiliki na akamatwe na kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Alifahamisha kuwa kuna taarifa ambazo amezipokea kuwa mmoja kati ya hao watuhumiwa ameonekena majira ya usiku bandarini akiwa anakimbia ndani ya Zanzibar.

"Tuna taarifa ambazo tumezipokea kuwa baadhi ya mtuhumiwa  wameonekana maeneo ya bandarini muda wa usiku akikimbia, mimi nataka kuwaambia  kuwa jeshi la polisi lipo macho kokote wanapokimbilia basi tutawatia nguvuni kwa ajili ya kuwachukulia hatua za kisheria" alieleza mkuu huyo wa Mkoa.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amewaomba wananchi kushirikiana na Serikali katika kutoa taarifa pindipo panapotokea ishara ya uvunjifu wa maadili na amani ya Nchi.

"Niwaombe wananchi kupitia vyombo vya habari kutoa ushirikiano  kwa serikali lakini pia kwa wale wenye video hizo zinazoonosha uvunjifu wa maadili uliofanywa katika Sherehe hiyo basi wazifute na wasisambaze kwani kuzisambaza kunatia aibu Zanzibar kwa vitendo hivyo" alisema Mkuu wa Mkoa.

katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amewataka Masheha wote ndani ya Mkoa huo kuzisimamia shughuli zote ambazo watatoa vibali vya upigaji wa musiki ili kusitokee vitendo vya uvunjifu wa maadili na udhalilishaji ndani ya mkoa huo.

"Ukweli kuwa Masheha ndio viongozi wa kila maeneo hivyo wanapotoa vibali vya upigwaji wa musiki basi kwanzia leo nawagiza wasimamie hadi pale mziki huo utakapo maliza muda wake" alisema RC Ayoub.

Alisema vitendo vingi vya uvunjifu wa maadili na udhalilishaji vinatokea katika hiyo miziki inayopigwa ambapo masheha ndio wanatoa vibali hivyo, Kwanzia sasa nawataka wasimamia hadi muda utakapo maliziaka.