Waandishi wa Habari waaswa kuripoti habari za Kitafiti


Waandishi wa habari nchini wamesisitizwa kutambua umuhimu wa kufuatilia habari za utafiti ili kutaarifu umma badala ya kuzikwepa na kujikita katika kuripoti habari za michezo, siasa, udaku na sekta nyingine pekee.

Hayo yalisemwa na Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya utafiti wa Mifugo Tanzania kwenye ofisi za Kanda inajumuisha mikoa ya Dar, Pwani Morogoro na Tanga, Dkt. Zabron Nziku wakati wa mafunzo kwa baadhi ya waandishi wa habari wa Kanda ya Mashariki na watafiti, yaliyoandaliwa na Tume ya Taifa ya sayansi na teknolojiakwa ufadhili wa shirika la Kimataifa la Maendeleo la Sweden (SIDA) yanayoendelea mjini Tanga.

Zabron alisema, lengo kubwa la mafunzo hayo ni kuona namna waandishi wa habari kuwajengea uwezo kuweza kushirikiana kati yao na watafiti .

Aidha wameaswa kushirikiana na taasisi zinazojuhusisha na tafiti mbalimbali ili waweze kupata taarifa sahihi kwa kutumia takwimu ili kuweza kuwahabirisha umma.

“Kwa sababu Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa viwanda hauwezi kuja bila kuwepo tafiti mbalimbali kwenye nyanja mbalimbali ikiwemo kilimo,mifigo,ardhi na maeneo mengine hivyo niipongeze Costec kwa kuja na mpango huo “alisema Zabron.

Alieleza kwani waandishi wa habari wamekuwa ni kiungo muhimu kati ya watu na wadau mbalimbali kuweza kupata taarifa sahihi za kuripoti kuhusiana na mambo ya utafiti.

Zabron alibainisha, watafiti wakitafiti na kupata matokeo mbalimbali yanaweza kuwa hayana tija kwa sababu yanatumia fedha kama hawajaweza kuwafikia walengwa na wadau mbalimbali wa hizo tafiti.

“Ambapo ninafanyia kazi tukiweza kutafiti namna bora au mifugo bora inayoweza kutoa maziwa kwenye ukanda wa Pwani huyo mnyama watabaki naye na taarifa zitabaki kituoni lakini kwa kuwatumia waandishi wa habari mnaweza kuzichukua taarifa sahihi zilizofanyiwa utafiti kuweza kuhabarisha jamii”alisema

Awali akizungumza wakati akiwasilisha mada kwenye mafunzo hayo ya Umuhimu wa Utafiti nchini Tanzania pamoja na umuhimu wa kusambaza matokeo ya utafiti,Afisa Utafiti Mkuu kiongozi kutoka Tume ya Sayansi na teknolojia Dkt Bakari Msangi aliwaomba waandishi wa habari wasikimbie watafiti na kuacha kuripoti habari za kiutafiti.

Alieleza, utafiti ni shughuli ya kutafuta uchunguzi ili kupata majibu yaliyopo.

“Utafiti ni shughuli ambayo ina mambo mengi ya uwekezaji kwa sababu unatumia fedha nyingi kuwasomesha watafiti na kuandaa maeneo ya utafiti na kufanya utafiti kwa kutumia gharama hivyo ni muhimu kuhakikisha kila ulichokipata kinatumika kuendelea ,kuongeza uzalishaji na tija kwa Taifa”alisema Msangi.