Wizara ya Kilimo yaahidi kushirikiana na wanajeshi wastaafu kuimarisha sekta ya kilimo



Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo_Dodoma

Serikali imewahakikishia Wanajeshi wastaafu kupitia muungano wa Wanajeshi Wastaafu Tanzania (MUWAWATA) kuwa imekusudia kuwashirikisha kwa karibu katika sekta ya kilimo kwani shughuli za kilimo zitaimarisha usalama wa chakula kwa kaya zao na Taifa kwa ujumla.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo leo tarehe 13 Novemba 2019 wakati wa ufunguzi ya mkutano wa semina ya mafunzo kwa muungano wa wanajeshi wastaafu Tanzania (MUWAWATA) uliofanyika tarehe 13 na 14 Novemba 2019 katika ukumbi wa Chama Cha Mapinduzi Jijini Dodoma (Dodoma Convention Center).

Aliongeza kuwa shughuli hizo zitaongeza kipato na kuboresha maisha ya wanajeshi hao kwa ujumla; Kuimarisha afya zao kwa kupunguza utegemezi wa ndugu, jamaa na marafiki kwa ajili ya kujikimu na maisha baada ya kustaafu.

Alisema kuwa Wizara ya Kilimo ipo tayari katika lengo la kufanya shughuli za kilimo kwa kutoa ushauri wa kitaalamu ikiwa ni pamoja na; kuwahakikishia upatikanaji wa mbegu bora, mbolea, zana za kisasa za kilimo na viuatilifu.

Mhe Hasunga amesema kwa kupitia Taasisi za Serikali na Mamlaka zilizopo, Wizara imeendelea kuboresha hali ya upatikanaji wa pembejeo kwa ujumla kwani ndio muhimili mkubwa katika sekta ya kilimo.

Kadhalika, amewahimiza wanajeshi hao na wakulima wote nchini kuzingatia matumizi bora ya pembejeo na kufuata ushauri wa kitaalamu, kwa kufanya hivyo ni Dhahiri kuwawataongeza tija na faida katika uzalishaji wa mazao ya kilimo.


Mhe Hasunga amesema kuwa sekta ya kilimo inachangia takribani asilimia 28.7 ya Pato la Taifa, asilimia 65.5 ya ajira, asilimia 65 ya malighafi ya viwanda na asilimia 30 ya mapato ya nje. Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) inatambua umuhimu wa ushirikishwaji wa wadau mbalimbali ili kuwezesha sekta na kilimo kuchangia kwa ufanisi katika ukuaji wa uchumi wa nchi na kuwezesha utekelezaji wa vipaumbele vya Taifa kwa ujumla.

Jitihada za Serikali zinalenga kuondoa vikwazo na changamoto za ukuaji wa sekta na kuimarisha Mapato ya Kilimo, kuboresha ukuaji wa mapato ya wakulima wadogo, kujitosheleza kwa chakula, uongezaji thamani ya mazao, ajira na hatimaye kufikia Nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.
Waziri Hasunga amesema kuwa lengo kuu la mkutano huo ni;  Kuwashirikisha wadau fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya kilimo ili kuongeza mchango wa sekta ya kilimo katika Pato la Taifa ikiwa ni pamoja na kuboresha maisha ya wakulima wadogo.

Amesema kuwa katika mkutano huo MUWAWATA wanapaswa kufanya wasilisho la shughuli za kilimo wanazozifanya na zile wanazotarajia kufanya kubainisha changamoto walizonazo na mapendekezo ya namna ya kutatua changamoto hizo.

Alisema kuwa matarajio ya mkutano huo ni pamoja na Kuongeza ufahamu (awareness creation) wa fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya kilimo, kupata fursa ya kuunganishwa na Wadau mbalimbali yakiwemo mabenki n.k.

Matarajio mengine ni Viongozi mbalimbali kutoka Serikalini na sekta binafsi kupata fursa ya kutoa maoni, ufafanuzi na kuwashauri MUWAWATA namna ya kushiriki katika kilimo; Kusikiliza changamoto zinazowakabili MUWAWATA na kuwashauri namna ya kuzitatua; na Kujenga uelewa kwa washiriki wa mkutano kuhusu Mikakati na Mipango ya Serikali katika kuiendeleza Sekta ya Kilimo.


Vilevile Waziri Hasunga ameitaja Programu ya kuendeleza sekta ya kilimo awamu ya pili (ASDP II) kuwa ni muhimu kwa wakulima nchini kwani inahimiza uongezaji thamani mazao ya kilimo kabla ya kuyauza ambapo pia itakuwa imeongeza nafasi za ajira kwa Watanzania.

Alisema hatua hiyo itaongeza ushindani wa bidhaa za ndani na nje ya nchi na itaiwezesha nchi kufikia malengo ya kuwa kwenye uchumi wa kati ifikapo 2025. “Ninawasihi MUWAWATA kujihusisha na kilimo kwa kuzingatia mnyororo wa thamani hasa kwa mazao ya vipaumbele ambayo yamebainishwa kwa kila eneo la kiikolojia” Alikaririwa Mhe Hasunga