Viongozi Zanzibar watakiwa kuhamasisha wananchi kushiriki chanjo ya vitamini 'A' na Minyoo


Wizara ya Afya Zanzibar imewataka viongozi wa ngazi za wilaya kisiasa na kidini kuwahamasisha wananchi kushiriki katika kampeni ya chanjo ya Matone ya Vitamin ‘A’ na minyoo inayotarajia kutolewa tarehe 5 hadi 31 mwezi huu.

 Akizungumza na Waandishi wa Habari Naibu Waziri wa Wizara hiyo Harusi Saidi Suleiman amesema utowaji wa matone hayo utafanyika katika vituo vyote vya afya pamoja na vituo maalum kwa siku ya Jumamosi na Jumapili.

Amesema katika kampeni hiyo zaidi ya watoto wenye umri wa miezi sita watapatiwa chanjo ya Vitamin ‘A’ na upimaji wa hali ya lishe na umri wa mwaka mmoja hadi mitano watapatiwa matone ya Vitamin ‘A’ na dawa za minyoo

Amesema lengo la serikali kuwahamasisha wananchi kutambua umuhimu wa kuwapeleka watoto wao vituo vya afya kwa kuwapatia chanjo hizo ili waweze kukua wakiwa na afya bora kuepukana na utapiamlo

 “Wananchi mshiriki katika kampeni hii kwa kuwapeleka watoto wanu  kupatiwa chanjo hiyo na dawa za minyoo ili kuokoa maisha yao na kukuwa katika afya njema,”alisema Naibu Waziri .

Nae Mkuu wa kitengo cha lishe Asha Hassan salmini amewataka wazazi na walezi kuvitumia vyakula vya asili vikiwemo matunda na mboga mboga kwa watoto wa umri ya chini ya miaka mitano kwa ajili ya kufikia mahitaji yao ya kupatiwa virutubisho vya nyongeza .

Aidha alisema kumnyonyesha mtoto maziwa ya mama kwa mpangilio kutasaidia ongezeko la vitamin mwilini mwao kwani maziwa ya mama yana vitamin vya aina zote

Kampeni ya chanjo ya matone ya Vitamin ‘A’ na dawa za minyoo hutolewa mwaka mara mbili ambapo mwaka huu zilianza Mwezi June na Kumalizia Disembar .