Katibu Mkuu Wizara ya Elimu atoa miezi miwili kukamilika kwa Shule ya Sekondari Patandi Arusha


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Tekinolojia Dkt. Leonard Akwilapo ametoa miezi miwili kukamilisha ujenzi Shule ya Sekondari maalum ya Wanafunzi Wenye Mahitaji Maalum ya Patandi mkoani Arusha.

Dkt.  Akwilapo ametoa maagizo hayo alipotembelea eneo la  mradi huo kuona hatua ya ujenzi  ilipofikia na kuridhishwa na kasi ya kazi inavyoendelea kupitia usimamizi wa Chuo cha Ufundi Arusha  (ATC )

"Ujenzi hapa ulikuwa hauendi kama tulivyotarajia kwa kasi na hata Ubora ,kwani usimamizi haukuwa mzuri  hivyo tutafanya maamuzi ya kubadilisha msimamizi  ili ikamilike na ujenzi ukamilike. Hivyo nimetoa miezi miwili watukabidhi shule ianze kutoa huduma" alisema Dkt Akwilapo.

Katibu Mkuu amesema ujenzi wa shule hiyo unasimamiwa na Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) baada ya kuwasimamisha Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) ambao walionyesha kusuasua katika usimamizi.

Dkt Akwilapo amesema wameshauriana na ATC na  kukubaliana kukamilisha shughuli zote za ujenzi ndani ya hiyo miezi miwili na kwamba tayari Wizara imetoa fedha zote zinazohitajika kwa ajili ya kukamilisha ujenzi huo zaidi ya Milioni Shilingi Milioni 500.

Aidha Kiongozi huyo ametoa wito kwa wazazi wote wenye watoto wenye mahitaji maalum wanaomaliza darasa la saba kuhakikisha wanawapeleka  shule za Sekondari  na kwamba  mzazi yeyote atakayemficha mtoto au kwenda kinyume atakuwa anaingia mgogoro na Serikali.

Naye Naibu Katibu Mkuu  Wizara ya Elimu  Dkt. Ave Maria Semakafu amesema Shule hiyo ambayo imejengwa katika Eneo moja na Chuo cha Ualimu wa Elimu Maalum cha Patandi  pia  Patandi kwa ajili ya  mazoezi  ya vitendo kwa wakurufunzi wa Chuo hicho na vingine pamoja na wanafunzi wa Vyuo vya  Elimu ya Juu wanaosomea ualimu wa Elimu maalum.


Mkuu wa shule hiyo mpya  Janeth Mollel amesema shule itakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi zaidi ya 400 ambapo wote watakaa Bweni.